Tanzania yapata mnunuzi wa tani laki moja ya Korosho kutoka Kenya

Serikali ya Tanzania kupitia Bodi ya Taifa ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko imesaini mkataba wa mauzo ya korosho ghafi kiasi cha tani laki moja kwa Kampuni ya Kenya ya ENDO Power Solutions kwa malipo ya Shilingi bilioni 418.

Mkataba huo umesainiwa jijini Arusha tarehe 30 Januari 2019 kati ya Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo Dkt. Hussein Mansoor kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na Bw. Brian Mutembei, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya ENDO Power Solutions ya nchini Kenya.

Tukio hilo la kihistoria lilishuhudiwa na Prof. Palamagamba Kabudi, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Joseph Kakunda, Waziri wa Viwanda na Biashara, Naibu Waziri wa Kilimo, Dkt. Innocent Bashungwa, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Prof. Florence Luoga, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Dkt.

Viongozi wengine walioshuhudia ni Balozi wa Kenya nchini, Mhe. Dan Kazungu, Prof. Sifuni Mchome, Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Prof. Joseph Buchweshaija, Katibu Mkuu wa Viwanda na Biashara, Prof. Siza Tumbo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Bw. Edwin Rutaberuka, Mkurugenzi wa TanTrade, Maafisa Waandamizi kutoka Serikalini na Waandishi wa Habari.

Awali wakizungumza kabla ya kusainiwa kwa Mkataba huo Mawaziri hao wakiongozwa na Prof. Kabudi, kwa pamoja walipongeza kwa dhati uamuzi wa Mhe. Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Serikali kununua korosho kutoka kwa wakulima ili kuepusha wakulima hao kuuza korosho zao kwa bei ya chini kwa watu wasio kuwa na nia njema kwa wakulima. 

Itakumbukwa kuwa, mwezi Novemba 2018, Mhe. Rais Magufuli alitoa maelekezo kwa Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo waratibu zoezi  la ununuzi wa korosho kutoka kwa wakulima kwa shilingi 3,300 kwa kilo moja.

Kwa upande wake Prof. Kabudi alisema kuwa anampongeza  Mhe. Rais Magufuli kwa uamuzi huo wa Serikali kununua korosho yote ili wakulima wapate bei inayolingana na jasho lao ambao hatimaye umezaa matunda kwa faida na maendeleo ya nchi.

Naye Mhe. Kakunda alieleza kuwa Bw. Mutembei ni mnunuzi wa kwanza kati ya wengi ambao walikuwa kwenye mazungumzo na Serikali kuhusu ununuzi wa korosho hizo. 

Mhe. Kakunda alisema katika majadiliano Serikali iliangalia kufanya biashara ya faida ambayo itawezehsa kulipa gharama mbalimbali ikiwemo gharama za upakiaji na upakuaji, malipo kwenye Serikali za Mtaa na michango mingine ya kijamii kwa mujibu wa makubaliano. 

Hivyo aliwataka watanzania na wenye viwanda kutokuwa na wasiwasi kwani Serikali ina nia njema ya kuwaletea maendeleo wananchi hususan kupitia sekta ya kilimo cha korosho.

“Wakulima wa Korosho wanatakiwa kumshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa uamuzi wake ambao unalinda maslahi ya mkulima na umewawezesha kuuza korosho zao kwa faida. Nawakaribisha wafanyabiasha makini kuja nchini kwani Serikali ipo tayari kuwasikiliza watu wa aina hiyo na kufanya nao biashara” alisema Mhe. Kakunda.

Kwa upande wake, Mhe. Bashungwa alieleza kuwa katika msimu wa korosho wa mwaka 2018/2019 tayari zimekusanywa tani 213,159 ambazo kati ya hizo tani 126,194 zimehakikiwa na tayari  wakulima wa mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma na Pwani wamelipwa fedha zao kwa zaidi ya asilimia 95.5. Mhe. Bashungwa aliongeza kuwa, mkakati wa Serikali ni kuhakikisha Wakulima wote kulipwa fedha zao hadi kufikia tarehe 05 Februari 2019.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Balozi wa Kenya nchini, Mhe. Kazungu alisema kuwa kusainiwa kwa mkataba huo ni faraja kubwa kwake katika historia ya mahusiano kati ya Tanzania na Kenya ambayo yanaendelea kuimarika siku hadi siku. 

Aidha, alieleza kuwa mkataba huo ni mfano mzuri wa kuimarika kwa mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki hususan katika masuala ya kilimo na biashara.

Kwa upande wake, mnunuzi wa korosho hizo ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Endo Powers Solutions, Bw. Mutembei alisema amekuja kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais Magufuli za kumwinua mkulima wa Tanzania na kwamba anawataka wale wote wanaobeza jitihada hizo za Mhe. Rais Magufuli kuacha mara moja huku akilaani kitendo cha baadhi ya wafanyabiashara kuendelea kuwakandamiza wakulima kwa kununua mazao yao kwa bei ndogo wanazopanga wao huku wakijua wazi kuwa wakulima hao wametumia gharama kubwa katika uzalishaji wa mazao hayo.

Pia aliwataka wafanyabiashara kufuata taratibu na sheria katika kufanya biashara kama Serikali zinavyoelekeza na kuacha kuchanganya biashara na siasa.

Naye Mkurugenzi wa Bodi ya Nafaka, Dkt. Mansoor alieleza kufurahishwa na tukio hilo ambalo limekuja wakati mwafaka wakati nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zikijiandaa na Mkutano wa Wakuu wa Nchi utakaofanyika jijini humo hivi karibuni. 

Aidha alisema kuwa, kwa kiasi kikubwa tukio hilo limeiinua Bodi yake na kwamba anatoa wito kwa wafanyabiasha wengine wa ndani na nje ya Tanzania kuja nchini na kushirikiana na Bodi hiyo ili kuwakomboa wakulima wengi Zaidi.

Mkataba huo umesainiwa wakati baadhi ya Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Tanzania wakiwa jijini Arusha kwa ajili ya kuhudhuria vikao vya maandalizi ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki utakaofanyika kwenye Kituo cha  Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) tarehe 1 Februari 2019.


from MPEKUZI

Comments