Taarifa Kutoka Jeshi La Polisi Mkoani Mbeya Leo

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linaendelea na jitihada za makusudi za kupiga vita wapiga ramli chonganishi @ lambalamba ambao kwa kiasi kikubwa wamekuwa wakisababisha madhara makubwa kwa jamii ikiwemo kuongezeka kwa matukio ya mauaji, kulipa kisasi na kuchochea chuki baina ya mtu na mtu au jamii na jamii.

Ikumbukwe kuwa, upigaji wa ramli chonganishi ni kinyume cha sheria ya tiba asili na mbadala namba 23 ya mwaka 2002. Wapiga ramli chonganishi @ lambalamba wengi wao hawana vibali vya kufanya shughuli hiyo, hivyo kukiuka sheria za nchi na kufanya matendo ambayo ni kinyume na haki za binadamu.

Kwa mujibu wa ibara ya 19 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 imekataza mtu mmoja au jamii kuingilia uhuru wa mtu mwingine katika imani, hivyo kutokana na baadhi ya watu kutokuwaamini wapiga ramli chonganishi jamii imekuwa ikihusika kwa kiasi kikubwa kuvunja sheria hii ya haki ya kuabudu.

Kwa kipindi cha mwezi Januari hadi Desemba, 2018 jumla ya wapiga ramli chonganishi waliokamatwa ni 78 kati yao wanaume ni 67 na wanawake 11.
  1. Jumla ya kesi zilizofikishwa Mahakamani [Fresh Case] – 29.
  2. Jumla ya kesi zilizoshinda Mahakamani [Conviction] – 10.
  3. Jumla ya kesi zilizoshindwa Mahakamni [Acquited] – 04.
  4. Kesi zilizo chini ya upelelezi [Progress Investigation] 02.
  5. Kesi zinazoendelea kusikilizwa Mahakamani [Preliminary Hearing] – 09.
Aidha Jeshi la Polisi Mkoani Mbeya linaendelea na mikakati mbalimbali ya kuzuia vitendo hivi visiendelee ikiwa ni pamoja na:-
 
Kupitia sera ya Polisi Jamii, kutoa elimu kwa wananchi kuhusu madhara ya imani potofu za kishirikina.
 
Kuendelea kushirikiana na Chama cha Waganga wa tiba asilia ili kuwabaini na kuwakamata wapiga ramli chonganishi hasa katika maeneo ambayo mara kwa mara vitendo hivi vimekuwa vikiripotiwa na kusababisha madhara kwa jamii husika.

Sambamba na hilo, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linatoa rai kwa wazazi na walezi kuongeza uangalizi kwa watoto wao hasa katika kipindi hiki cha mvua zinazoendelea kunyesha hapa nchini kadhalika na kuweka uangalizi wa kutosha hasa kutokana na mkoa jirani wa Njombe kuripotiwa kwa matukio ya kupotea kwa watoto na hata wengine kupatikana wakiwa wamekufa kutokana na kinachodaiwa ni kuwepo kwa imani za kishirikina.
 
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linaendelea kutoa wito kwa wananchi kutoa taarifa za mtu au watu wanaowatilia mashaka katika maeneo yao ili uchunguzi zaidi uweze kufanyika dhidi yao. Aidha Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limechukua tahadhari kwa kufanya doria katika maeneo mbalimbali pamoja na kuunda dawati maalum la ulinzi wa mtoto kwa kushirikiana na idara nyingine za serikali ili kuhakikisha watoto wanapata ulinzi wakati wote.
 
Imetolewa na:
[ULRICH OMATEI – SACP]
KAMANDA WA POLISI MKOA WA MBEYA.


from MPEKUZI

Comments