Spika Ndugai, Zitto Kabwe Mahakamani Leo

 Kesi ya kikatiba kuhusu kinga ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kwa mujibu wa Katiba ya Nchi na Mamlaka ya Bunge katika kuwaita na kuwahoji watu mbalimbali, leo inatajwa rasmi mahakamani.

Kesi hiyo ya Kikatiba namba 01/2019 imefunguliwa Mahakama Kuu, Masjala Kuu na mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe dhidi ya Spika wa Bunge, Job Ndugai.

Mahakama hiyo imetoa wito kwa wadau wote (mdai- Zitto na mdaiwa-Spika) ikiwataka kufika mahakamani leo kesi hiyo itakapotajwa kwa mara ya kwanza.

Kesi hiyo imepangwa kusikilizwa na jopo la majaji watatu wakiongozwa na Firmin Matogolo, Dk Benhajj Masoud na Elinaza Luvanda.

Katika kesi hiyo, Zitto ambaye pia ni Kiongozi wa Chama cha ACT- Wazalendo anaiomba Mahakama Kuu itoe tafsiri ya kinga ya CAG iliyopo kikatiba na tafsiri ya Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge katika kushtaki watu wanaosemekana kulidharau Bunge.

Zitto alifungua kesi hiyo baada ya Spika kupitia kwenye vyombo vya habari na baadaye kumwandikia barua CAG, Profesa Mussa Assad akimtaka afike mbele ya kamati ya Bunge kuhojiwa kutokana na kauli aliyoitoa akiwa Marekani kuwa Bunge ni dhaifu.


from MPEKUZI

Comments