Kiongozi wa Upinzani Venezuela Aliyejitangaza Rais Afanya Mazungumzo na Wanajeshi

Kiongozi wa upinzani nchini Venezuela Juan Guaidó amefanya mazungumzo ya siri na wanajeshi kutafuta uungwaji mkono wao wa kumng'atua madarakani rais Nicolás Maduro.

Mwezi uliyopita Bw. Guaidó alijitangaza kuwa rais katika hatua ambayo imeungwa mkono na Marekani na mataifa kadhaa ya Amerika kusini.

Mataifa ya Urusi na China yanamuunga mkono Maduro lakini msaada wa jeshi ni muhimu kwa juhudi zake za kusalia madarakani.

Mzozo ulianza baada ya Bw. Nicolás Maduro kuanza muhula wa pili madarakani licha ya uchaguzi kukumbwa na mzozo.

Wagombea wengi wa upinzani walizuiliwa kushiriki uchaguzi huo na wengine kufungwa jela.
 
Karibu watu milioni tatu wametoroka nchini Venezuela kufuatia mzozo wa kiuchumi huku taifa hilo likikumbwa upya na ghasia hivi karibuni.

Rais wa Marekani Donald Trump, siku ya Jumatano aliandika katika mtandao wake waTwitter kuwa amezungumza na Bw. Guaidó na kwamba anaunga mkono "Urais wake wa kihistoria", aliandika katika ujumbe wake wa pili kuwa "Harakati za kupigania uhuru zimeanza!"
 
Waziri wa mambo ya nje wa Uingereza Jeremy Hunt, anatarajiwa kuyashawishi mataifa ya Muungano wa Ulaya kuwaekea vikwazo maafisa wa ngazi ya juu katika serikali ya Bw. Maduro leo Alhamisi baada ya kuzungumza na Bw. Guaidó siku ya Jumatano.

Credit: BBC


from MPEKUZI

Comments