Wema Sepetu Apewa Masharti Na Familia

Baada ya kuanzisha biashara yake ya duka la nguo za watoto liitwalo 'Little Sweetheart', staa wa kike wa sinema za Kibongo, Wema Sepetu amepewa masharti na familia yake namna ya kuliendesha duka hilo, pamoja na kuachana na baadhi ya marafiki wasiokuwa na faida kwake.
 
Miongoni mwa masharti aliyowekewa Wema na familia yake ni kuwa chini ya dada yake aitwaye Nuru Sepetu. Nuru ndiye meneja wa Wema kwa sasa hivyo ili kumfikia staa huyo lazima upite kwake.

“Nuru ndiye anayesimamia kila kitu dukani hapo kuliko kumwachia Wema mwenyewe ambaye wanamjua ana mambo mengi hivyo usimamizi unaweza kumshinda na hata huyo Wema mwenyewe lazima afuate maelekezo ya Nuru", kimesema chanzo hicho na kuongeza;

“Wema anatakiwa kujilinda na skendo kwani kadiri atakavyokuwa akichafuka ndivyo atakavyokuwa akiharibu taswira ya biashara kwa maana ya jina la duka na ameambiwa kama akileta mambo yake ya skendo za kila kukicha, basi atapoteza hata wateja hivyo lazima ajilinde na alinde jina lake kubwa ambalo amekuwa akishindwa kulitumia kwa muda mrefu kumwingizia pesa".

Mbali na hayo, Wema pia amepigwa marufuku kufanya mahojiano ya mara kwa mara na vyombo vya habari ambavyo vingine vimelenga kumharibia badala ya kumjenga. 

“Sasa hivi hatakiwi kabisa kuzungumza na waandishi wa habari, badala yake anayetakiwa kuzungumza kwa niaba yake ni Nuru ambaye ndiye msemaji wake".

Duka hilo la Wema lililopo Kinondoni jijini Dar es salaam, ni la pili baada ya lile la kwanza lililomshinda, ambalo lilikuwa likiuza lipstick zake za 'Kiss by Wema' lililokuwa maeneo ya Mwenge, jijini humo.


from MPEKUZI

Comments