Mtumishi benki ya NMB Ajeruhiwa Jijini Mbeya....Watu 9 Watiwa Mbaroni

Watu tisa wamekamatwa Mkoani Mbeya kwa tuhuma za uhalifu wa kuvunja, kuiba na kujeruhi likiwemo tukio la mtumishi wa benki ya NMB Kasumulu Kyela na mkazi wa Iwambi Jijini Mbeya Habib Juma.
 
Kamanda wa Polisi Mkoani Mbeya Ulrich Matei amewataja watuhumiwa wawili waliomjeruhi mtumishi wa NMB ni Richard Jackson fundi ujenzi mkazi wa DDC Mbalizi na David Labi (32) ambao walikamatwa Disemba 9 mwaka huu majira ya saa nane mchana wakiwa na nguo za majeruhi, TV, Simu aina ya Tecno na vifaa vilivyotumika kumshambulia majeruhi.
 
Matei alisema watuhumiwa wamekiri kutenda uhalifu huo na kuonesha vitu vilivyoibiwa pamoja na bomba lililotumika kumpigia kichwani ambapo hivi sasa majeruhi anapatiwa matibabu Jijini Dar es Salaam.
 
Aidha Kamanda Matei alisema Disemba 13 mwaka huu Jeshi la Polisi limefanikiwa kuwakamata watu sita kwa tuhuma za kuwavamia watu usiku wakijifanya sungusungu hususani maeneo ya TEKU, Ilomba,Ituha na VETA.
 
Matei alisema kinara wa tukio hilo ni Pascally Aron (18)dereva wa Bajaj na mkazi wa Ilemi Jijini Mbeya. Wengine ni Justin Laurence(18) fundi ujenzi mkazi wa Ilemi, Allen Daud(19)mkulima mkazi wa Ilemi, Yassin Naso(19) mkazi wa Ilemi, Hamza Charle (22)mkazi wa Ilemi na Anthony Elias (32)mkazi wa Ilemi. 

Pascally alikiri kujihusisha na uhalifu kwa kujifanya sungusungu ambapo hutishia kwa kutumia mapanga na kuwapora watu vitu vya thamani.
 
Hata hivyo alisema baada ya uchunguzi kukamilika watuhumiwa watafikishwa mahakamani.
 
Alitoa wito kwa yeyote mwenye kufahamu makundi yanayojihusisha na uhalifu kuwasiliana na jeshi la pilisi kupitia ulinzi shirikishi.


from MPEKUZI

Comments