Mrema Aiangukia Serikali Ruzuku Vyama vya Siasa .....Aiomba Iruhusu Mikutano ya Hadhara

Mwenyekiti wa Chama cha TLP, Augustino Mrema, ameitaka serikali inapofanya marekebisho ya vyama vya siasa kuangalia umuhimu wa kuvipatia vyama vidogo vya siasa ruzuku, ili navyo viweze kujiendesha.
 
Mbali na kutaka marekebisho hayo kuruhusu vyama vya siasa ambavyo havina wabunge wala madiwani kupewa ruzuku, pia ametaka sheria iruhusu kufanyika kwa mikutano ya siasa ili kuweza kujenga vyama hivyo.
 
Mrema alitoa kauli hiyo alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma jana na kusema yapo mambo ambayo katika marekebisho ya siasa lazima yaingizwe na kutoa nafasi sawa kwa vyama vya siasa vidogo na vikubwa, kwani
vyote vinafanya siasa za kulijenga taifa kwa misingi ya utaifa.
 
Katika hatua nyingine Marema alivitaka vyama vya siasa vya
upinzani kuangalia uwezekano kwa kuunganisha nguvu kwa ajili ya kuusoma vema muswada wa vyama vya sheria na kuona ni wapi kuna mapungufu, ili yaweze kurekebishwa na yale mazuri yakubaliwe.
 
Mrema ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Parole, alisema
licha ya kuwa yeye ni mtumishi wa serikali kwa sasa, hawezi kufumbia macho mambo maovu ambayo yanafanywa na serikali na kama yatakuwepo atayasema.
 
“Mimi pamoja na kuwa mtumishi wa serikali ikumbukwe nimeitumikia nchi hii kwa nafasi mbalimbali, hivyo siwezi kunyamaza pale ninapoona mambo yanaenda vibaya, lakini pia ninapoona mambo yanaenda vizuri nitasema ukweli,”alisema Mrema.
 
Mrema alikana kuwa kibaraka wa serikal, ila  akasema anapenda kusimamiaukweli. 

“Siyo kweli kuwa mimi ni kibaraka wa serikali ya CCM ila nataka kufanya siasa ambayo inaweza kuwa na tija. Haiwezekani nikaona serikali inafanya vibaya nikanyamaza, lazima nitasema na kuikosoa serikali,” alisema na kuongeza:
 
“Kwa mfano nataka serikali iruhusu mikutano ya kisiasa kwa
vyama vyote vya siasa kwani vyama vyote vinajenga nchi, lakini pia ikumbukwe kuwa vyama vyote vinatakiwa kupewa ruzuku ili viweze kujiendesha,” alisema Mrema.


from MPEKUZI

Comments