Mapendekezo Yaliyotolewa na THTU kwa Rais Magufuli kuhusu kikokotoo

Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu (THTU), Paul Loisulie ametoa pendekezo la kuundwa kwa  kamati shirikishi kwa ajili ya kujadili na kusikiliza hoja kuhusu kikokotoo.

Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Desemba 28, 2018 mbele ya Rais John Magufuli Ikulu jijini Dar es Salaam katika mkutano unaoendelea hivi sasa uliowakutanisha viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta), mifuko ya hifadhi za jamii ya PSSSF na NSSF na Mamlaka ya Usimamizi wa Hifadhi ya Jamii (SSRA).

Hivi karibuni umeibuka mjadala kuhusu mafao baada ya kanuni  za Usimamizi wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kuondoa mfumo wa zamani wa kulipa asilimia 50 ya mafao ya mkupuo na badala yake mstaafu kuruhusiwa kuchukua asilimia 25 kwa mkupuo na asilimia 75 igawanywe ili ilipwe kama pensheni kwa kila mwezi kwa kipindi chote cha maisha ya mstaafu.

Katika maelezo yake Loisulie amesema kamati hiyo itakwenda kufanya hesabu ya kusikiliza hoja za wafanyakazi na mwelekeo bora zaidi kuhusu suala hilo ili waende kisayansi.

“Ninaamini tukikaa pamoja na kuangalia msingi wa  kikotoo hiki tutapata mwafaka ambao hautaumiza mifuko wala wafanyakazi,”  amesema.

Amesema moja ya madai ya wafanyakazi baada ya mifuko kunganishwa ni kupata mafao madogo tofauti na ilivyokuwa hapo awali.

Amesema mbali na hilo, wafanyakazi wanataka itumike fomula ya mwanzo ilivyokuwa mifuko mbalimbali lakini msimamizi hataki kwa madai ya kuwa mifuko itakufa badala yake itumike mpya.

Kikao hicho kinaongozwa na Rais Magufuli ambaye huenda akaweka msimamo wake kuhusu sakata hilo.


from MPEKUZI

Comments