Serikali Yajadili Uwekezaji Bora Zaidi Wa Misri Katika Sekta Ya Mifugo

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Luhaga Mpina ameongoza kikao cha wakuu wa idara zilizo chini ya wizara yake pamoja na wadau wengine wa sekta ya mifugo, kujadili namna bora zaidi ya serikali ya Tanzania inavyoweza kunufaika na uwekezaji katika sekta ya mifugo kutokana na nia ya serikali ya Misri kutaka kuwekeza katika sekta hiyo iliyooneshwa katika siku chache zilizopita.

Akizungumza katika kikao hicho kilichofanyika ofisi ndogo za wizara hiyo Jijini Dar es Salaam, Mhe. Waziri Mpina amewaambia wajumbe wa kikao hicho wakiwemo wawakilishi kutoka SUMA JKT, Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) na Dawati la Sekta Binafsi, kuwa na mikakati ambayo itasaidia uwekezaji huo uwe na tija kwa taifa.

Aidha Waziri Mpina amesema serikali inahitaji wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi, lakini ni muhimu yakaandaliwa mazingira bora zaidi ili uwekezaji huo uwe endelevu na kuleta tija kwa taifa na wananchi kwa ujumla.

Baadhi ya wajumbe waliohudhuria kikao hicho, wamemshauri Mhe. Waziri Mpina masuala mbalimbali yakiwemo ya kitaalam pamoja na vifungu vya kisheria ili mikataba itakapoandaliwa na kusainiwa kati ya serikali ya Tanzania na Misri iweze kuleta faida kwa nchi hizo mbili.

Hivi karibuni Kaimu Balozi wa Misri nchini Bibi. Neville El-Saeed na Mkuu wa kitengo cha Uchumi katika ubalozi huo Bw. Mohamed Ibrahim, walifika katika ofisi ndogo za wizara hiyo katika siku tofauti tofauti ambapo walipata fursa ya kuzungumza na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Luhaga Mpina kuhusu uwekezaji huo.

Maafisa hao pia walikutana na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel na kumkabidhi andiko la awali la nia ya serikali ya nchi hiyo kutaka kuwekeza katika sekta ya mifugo na kufungua fursa zaidi zilizopo katika sekta hiyo.


from MPEKUZI

Comments