Mmiliki Wa Leicester City Afariki Dunia Ndani Ya Helikopta Yake Iliyoteketea Kwa Moto

Klabu ya Leicester City ya nchini Uingereza imetangaza rasmi kuwa mmiliki wa klabu hiyo raia wa Thailand, Vichai Srivaddhanaprabha amefariki dunia katika ajali ya helikopta nje ya uwanja wa klabu hiyo, King Power.

Bosi huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa klabu hiyo alikuwa ni mmoja kati ya watu watano waliopoteza maisha katika ndege hiyo, ajali iliyotokea Jumamosi ya wiki iliyopita.

Ndege hiyo ilitua katika eneo la kuegesha magari karibu na uwanja, muda mfupi baada ya kuruka, mara bada ya kumalizika kwa mchezo wa Leicester City na West Ham United, mchezo ambao timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1.

Taarifa rasmi ya Leicester City, imesema: "Katika hali ya kuhuzunisha na kuumiza, tunathibitisha kwamba Mwenyekiti wetu, Vichai Srivaddhanaprabha alikuwa ni mmoja ya watu waliopoteza maisha  Jumamosi jioni baada ya helicopta iliyombeba pamoja na watu wengine wanne kuanguka nje ya uwanja wa King Power".

Srivaddhanaprabha aliinunua Leicester City mwezi Agosti 2010 kwa dau la Pauni millioni 39 na kisha kuchaguliwa kuwa mwenyekiti wa klabu mwaka 2011.

Alikuwa nyuma ya mafanikio ya Leicester City iliyoshangaza ulimwengu kwa kushinda ubingwa wa ligi kuu nchini Uingereza (EPL) msimu wa 2015/16 chini ya kocha, Claudio Ranieri.

Kwa mujibu wa jarida la Forbes, Srivaddhanaprabha amecha utajiri ukaokadiriwa thamani ya Dola bilioni 4.9, utajiri ambao umemfanya kuwa katika nafasi ya 15 ya listi ya matajiri nchini Thailand.


from MPEKUZI

Comments