Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan Awataka Watanzania Kumuenzi Baba wa Taifa Kwa Kuwekeza Katika Viwanda

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan amewataka Watanzania kumuenzi baba wa Taifa hayati Mwl. Julius Nyerere kwa kuwekeza katika viwanda ili nchi irejee katika uchumi wa kutegemea uzalishaji unaotokana na bidhaa za viwandani.

Ameyasema hayo leo Jumatatu Oktoba 29, katika uzinduzi wa wiki ya maonesho ya viwanda yaliyofanyika katika viwanja vya Sabasaba Picha ya Ndege Kibaha mkoani Pwani na yatafungwa Novemba Nne mwaka huu ambapo wamiliki na wafanya biashara wa bidhaa zitokanazo na viwanda vya hapa nchini watapata fursa ya kuzionesha.

Amesema katika mkoa wa Pwani kuna viwanda 429 ambavyo kati ya hivo vipo vikubwa, vya kati na vidogo ambavyo vimejengwa na vingine vishaanza uzalishaji japo kuna changamoto za soko la bidhaa hizo kwasababu uzalishaji ni mkubwa kuliko uuzaji.

“Tunategemea maonesho haya yatakuwa endelevu kwasababu viwanda hivi vinatoa ajira kwa watanzania ni matumaini yangu kuwa wafanyabiashara mtatumia fursa hii kukuza biashara zenu,  tulipotembelea baadhi ya viwanda wamiliki wageni wanataka kuondoka na kuachia uongozi na uendeshaji kwa wazawa.

“Nasisitiza kuendelea kuwepo kwa mshikamano kati ya wizara ya viwanda na biashara na  sekta binafsi ili uwekezaji ukue zaidi ya hapa na bidhaa zinapouzwa nje na zikiwa na nembo yenye kuonyesha ni bidhaa zilizotengenezwa hapa nchini ni fursa yetu ya kujitangaza, ” amesema.

Aidha ametoa rai kwa Wizara ya na Ajira na sekta zinazosimamia masuala ya  Kazi kutembelea viwanda hivyo ili kujionea jinsi wafanyakazi wanaendesha kazi zao na kujua  kama haki zao za kisheria zinafatwa kwasababu kuna maeneo aliyotembelea watu wanafanya kazi zaidi ya masaa yaliyowekwa na serikali kikatiba.


from MPEKUZI

Comments