Kesi Ya Walimu Wanaotuhumiwa Kuiba Mitihani Darasa la 7 Yapigwa Kalenda Hadi Octoba 24

Upelelezi wa kesi ya kupata mitihani ya taifa ya darasa la saba inayowakabili walimu watano wa shule ya msingi ya kimataifa ya Hazina iliyopo Magomeni katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu bado haujakamilika.

Wakili wa Serikali, Mwanaamina Kombakono aliyaeleza hayo jana Oktoba 10, 2018 mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi.

Kombakono alidai mahakamani hapo kesi ilipangwa kwa ajili ya kutajwa na upelelezi wake bado haujakamilika na akaomba ipangiwe tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.

Baada ya kutolewa maelezo hayo, Hakimu Shaidi aliiahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 24, 2018.

Washtakiwa hao watano wanaokabiliwa na kesi hiyo ni Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo ya Hazina, Patrick Cheche (43), mkazi wa Mapinga Bagamoyo na walimu wake Laurence Ochien (30), Justus James (32), Nasri Mohamed (32) na Mambo Idd (32).

Washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka ya kula njama ya kuingilia mitihani ya Taifa, kupata na kuwaonyesha watahiniwa maudhui ya mtihani na kufanya mawasiliano na watahimiwa.


from MPEKUZI

Comments