NGOs Zapewa Mwezi Mmoja Kuwasilisha Taarifa Za Matumizi Ya Fedha Kwa Msajili

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeyaagiza Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini kuwasilisha kwa Msajili wa Mashirika hayo taarifa za fedha zilizokaguliwa za mwaka 2016 na 2017 ndani ya siku thelathini kuanzia leo Septemba, 28, 2018.

Hayo yamesemwa leo jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya masuala mbalimbali yanayuhusu Usajili na Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini.

Dkt. Ndugulile  ameyataka pia Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kuwasilisha taarifa inayoonesha miradi iliyotekelezwa kwa fedha iliyopatikana  kwa mwaka wa 2016 na 2017 na kutoa taarifa ya vyanzo vya mapato husika ikiambatana na hati za makubaliano za vyanzo husika kwa kipindi cha miaka hiyo.

Naibu Waziri Dkt. Ndugulile ameeleza kuwa Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya mwaka 2001 inasisitiza misingi ya uwazi na uwajibikaji kwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini.

Amesisitiza  kuwa kwa mujibu wa Kifungu cha 29(a) na (b) cha Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Na. 24 ya mwaka 2002, Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yana wajibu wa kuwasilisha taarifa za kazi na fedha kila mwaka kwa Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na kwa Umma.

Ameongeza kuwa Kanuni za utendaji za Mashirika Yasiyo ya Kiserikali za mwaka 2008 zinasisitiza uzingatiaji wa misingi ya uwazi na uwajibikaji katika utendaji kazi, masuala ya fedha na utawala hivyo wanufaika wa miradi yao, Halmashauri wanapofanya miradi na vyombo vya habari wana haki ya kupata taarifa hizo.

Dkt. Ndugulile ameeleza kuwa pamoja na kuwepo kwa miongozo hiyo bado Mashirika Yasiyo ya Kiserikali mengi yamekuwa yakikiuka matakwa husika hivyo kuleta mkanganyiko katika jamii.

“Serikali itaendelea kufuatilia na haitosita kuchukua hatua kali za kisheria ikiwemo kuzifutia usajili NGOs ambazo zitashindwa kutekeleza agizo hili ndani ya muda uliopangwa” alisisitiza Dkt. Ndugulile.

Pia Dkt.Ndugulile ameziagiza NGOs nchini zizingatie ushiriki wa wazawa wa ndani katika miradi wanayoitekeleza kwa mujibu wa Sheria, kanuni na taratibu za uendeshaji wa shughuli za NGOs hapa nchini.

Aidha Dkt. Ndugulile ameyataka Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kutuma taarifa zao za fedha na za miradi kila mwaka kama ilivyoagizwa kupitia barua pepe ifuatayo dngo@communitydevelopment.go.tz .

Maagizo haya kwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yanakuja siku chache mara baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kumuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, JInsia, Wazee na Watoto (anayeshughulikia Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto) Dkt. John Jingu kufuatilia utendaji kazi wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini wakati alipokuwa akimuapisha kuwa Katibu Mkuu huyo katika Ikulu ya Chamwino Dodoma.


from MPEKUZI

Comments