Vigogo Benki Ya Posta Watupwa Jela Miaka Mitano.

VIGOGO wawili wa Benki ya Posta Tawi la Tabora na mfanyabiashara mmoja  waliokuwa wanakabiliwa na jumla ya mashitaka saba ikiwemo utakatishaji wa zaidi ya shilingi milioni 700 wametupwa jela miaka mitano au kutakiwa  kulipa faini ya shilingi milioni mia moja (100).

Mbali ya adhabu hiyo Mahakama hiyo baada ya kuwatia hatiani  imewataka  washitakiwa hao kulipa shilingi milioni 710 walizoziibia Benki ya Posta na vinginevyo mali zao zitaifishwe na serikali kufidia kiasi cha fedha zilizoibwa.

Uamuzi wa shauri hilo la jinai namba 154/2015 umetolewa jana na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Tabora Jocktan Rushwela baada ya kuwatia hatiani washitakiwa hao kwa makosa matatu kati ya saba.

Vigogo wa benki ya Posta  Tabora waliopata adhabu hiyo ni Boaz Lunyungu aliyekuwa meneja, George Ngatunga(mhasibu) na mfanyabiashara Umaiya Makiliga.

Katika hukumu hiyo iliyosomwa kwa saa mbili  Hakimu Rushwela aliwatia hatiani watuhumiwa hao kwa makosa matatu kati ya saba waliyokuwa wanashitakiwa nayo ambayo ni kula njma ya kutnda kosa la wizi, kutakatisha fedha na wizi.

Awali upande wa mashitaka ukiongozwa na wakili mwandamizi wa Serikali Shedrack Kimaro aliiambia Mahakama hiyo kuwa watuhumiwa walitenda makosa hayo kati ya Januari 2014 na julai 2915 katika benki ya posta tawi la Tabora.

Wakili Kimaro alidai  kwenye shitaka la kwanza kuwa katika kipindi hicho washitakiwa kwa pamoja walikula njama ya kutenda kosa la wizi.

Ilidaiwa na wakili Kimaro kuwa washitakiwa wote watatu katika tarehe tofauti kati ya mwezi Januari 2014 na mwezi julai 2015 waliiba jumla ya shilingi milioni 710 katika benki ya Posta tawi la Tabora.

Shitaka la tatu ambalo lilikuwa likiwakabili aliyekuwa meneja na Mhasibu wake ilidaiwa kuwa wakiwa ni watumishi wa benki wa Posta walitakatisha fedha shilingi milioni 710 huku wakijua wamezipata kwa njia zisizo halali.

Upande wa jamuhuri wakati wa usikilizwaji wa shauri hilo ulileta jumla ya mashahidi 16 ambao waliweza kutoa ushahidi uliopeleka mahakama kuthibitisha pasipo shaka kwamba watuhumiwa walitenda makosa hayo.

Mahakama imewahukumu kwenda jela miaka mitatu mitatu kwa kosa la kula njama na lile la wizi na miaka mitano kwa kosa utakaktishaji wa fedha, kwa vile adhabu hizo zinakwenda pamoja watutumikia kifungo cha miaka mitano jela.

Washitakiwa hao watatu pamoja na kupata adhabu hiyo ya kifungo bado wanakabiliwa na kesi nyingine ya kuhujumu uchumi wakiwa na watu wengine 13 shauri amabalo bado halijaanza kusikilizwa kwani jalada lake lipo ofisini kwa DPP likisubiri kutolewa uamuzi.


from MPEKUZI

Comments