Sekta ya Mifugo Kuchochea Ujenzi wa Uchumi wa Viwanda

Frank Mvungi- MAELEZO, Dodoma
Serikali imepanga  kuzalisha mitamba zaidi ya milioni 1  kwa mwaka ili kukuza sekta ya mifugo hapa nchini ili  kuchochea ujenzi wa uchumi wa  viwanda.

Akizungumza  katika kipindi maalum cha TUNATEKELEZA kinachorushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) na kuratibiwa na Idara ya Habari- MAELEZO, Waziri wa Mifugo na Uvuvi  Mhe. Luhaga Mpina amesema kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa sekta hiyo inatoa mchango mkubwa katika ujenzi wa uchumi na ustawi wa wananchi.

“Vituo vya uhaulishaji vilivyopo Arusha na Sao Hill Iringa vimeboreshwa ili viweze kutoa mbegu bora za kutosha kwa kufanya maboresho makubwa katika vituo  vya kanda vya uzalishaji mbegu za mifugo” alisisitiza Mpina

Amesema kuwa kuelekea uchumi wa viwanda, Serikali imejipanga kuzalisha mifugo mingi ya kutosha ili kupata bidhaa bora zitokanazo na mifugo, Aliongeza kuwa Serikali imevunja mikataba na wawekezaji wengi ambao hawakuweza kutimiza malengo ya uwekezaji katika sekta ya mifugo.

Katika kuboresha sekta ya uvuvi Waziri Mpina amesema wafanyabiashara watumie fursa ya kuzalisha nyavu halali ili kuchochea ukuaji wa sekta ya uvuvi kwa kuwa kuna mahitaji makubwa ya bidhaa za uvuvi.

Pia aliwaasa Viongozi wote wa Serikali kutojiusisha na uvuvi haramu kwani ni kinyume na taratibu za utumishi wa umma.

Katika kuimarisha sekta ya mifugo amesema kuwa Serikali imeendelea kukusanya madeni yanayodaiwa na NARCO  ambapo  zaidi ya bilioni 3 zimekusanywa.

Kipindi cha ‘TUNATEKELEZA’ kinarushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) na kuratibiwa na Idara ya Habari MAELEZO kikiwashirikisha Mawaziri wote  kwa awamu hii.


from MPEKUZI

Comments