Ripoti LHRC: Wanawake 203 hubakwa kila mwezi

Kituo cha sheria na haki za binadamu (LHRC) kimetoa ripoti ya hali ya haki za binadamu kwa kipindi cha miezi sita kuanzia mwezi Januari hadi Juni, 2018 ambapo matukio ya ukatili kwa wanawake yameongezeka ikilinganishwa na mwaka jana.

Akizungumza na wanahabari Mkurugenzi mtendaji wa LHRC Anna Henga, amesema kuwa kwa kipindi cha kuanzia Januari 2018 hadi Juni 2018, idadi ya wanawake 1,218 wameripotiwa kubakwa, inakadiriwa ni wanawake 203 kila mwezi, huku mauaji ya kujichukulia sheria mkononi yamepungua.

“Kwa kipindi cha kuanzia Januari 2018 hadi Juni 2018, matukio ya kujichukulia sheria mkononi na mauaji ya kwa imani za kishirikina yamepungua kutoka 172 hadi 106”, amesema Henga.

Henga ameongeza kuwa hofu ya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi imeongezeka kuelekea kwenye uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2020 lakini hakuna tukio la mauaji lililoripotiwa kuanzia Januari hadi Juni mwaka huu.

Kwa mujibu wa LHRC katika ripoti yake ya Mwaka 2017 wanawake walifanyiwa aina mbalimbali za ukatili ikiwemo wa kimwili na kingono. Huku takwimu za Jeshi la Polisi zinaonyesha kwamba jumla ya kesi za ubakaji 2,059 ziliripotiwa kufikia mwezi Machi 2017 na kufikia mwisho wa Disemba 2017, matukio ubakaji yalikuwa 8,039, yakiongezeka kwa kiwango kikubwa (matukio 394), ukilinganisha na matukio 7,645 ya mwaka 2016 .


from MPEKUZI

Comments