Katibu Mkuu CCM Amtolea Uvivu Waziri Anayemiliki Heka 1000 za Ardhi Morogoro

Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally amesema amemuita mmoja wa mawaziri wa Serikali ya Awamu ya Tano aeleze alipopata ekari 1,000 za mashamba.

Bila kumtaja jina waziri huyo, Dk Bashiru amesema atamtaka achague jambo moja kati ya kuwa mporaji ama kiongozi wa chama hicho.

Ametoa kauli hiyo jana Alhamisi Agosti 30, 2018 wakati akifungua mkutano wa Baraza la Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi (UWT) Taifa jijini Dodoma.

Amesema mambo yanayozungumzwa katika vyombo vya habari unaweza kudhani ndio hali halisi katika Jamii.

"Viongozi msifanye kazi katika vyombo vya habari nendeni katika maeneo mbalimbali mkatatue kero za wananchi. Nilikwenda eneo moja wananchi wanajiuliza waziri huyo amepataje ardhi hiyo," alisema Dk Bashiru.

Alisema atamuita waziri huyo aeleze amepataje eneo hilo kwa sababu CCM haiwezi kuwa na wanachama ambao ni waporaji wa ardhi.

“Achague kimoja kama ni mporaji ama kuwa kiongozi wa CCM," alisisitiza.



from MPEKUZI

Comments