Waziri Mkuu Asema Ukaguzi Kwenye Kizuizi Cha Uvinza Ni Endelevu.....Asema lengo ni kudhibiti uingizwaji wa silaha haramu nchini

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwaamesema ukaguzi wa watu na mizigo unaofanywa kwenye kizuizi cha Uvinza mkoani Kigoma utaendelea kufanyika ili kudhibiti wimbi la uingizwaji wa silaha haramu nchini.

“Lazima ukaguzi ufanyuke ili kujiridhisha kama watu wote wanaoingia nchini wamepita kihalali na kama hawapitishi silaha haramu na vitu vingine ambavyo haviruhusiwi kuingizwa nchini,”.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumapili, Julai 29, 2018) wakati akizungumza na wananchi wa wilaya ya Uvinza akiwa katika siku ya pili ya ziara yake ya kikazi mkoani Kigoma.

Ametoa ufafanuzi huo baada ya Mbunge wa jimbo la Kigoma Kusini, Bibi Hasna Mwilima kudai kuwa wananchi wengi wanapata usumbufu mkubwa kutokana na ukaguzi unaofanywa na Maafisa wa Uhamiaji katika kizuizi cha Uvinza.

Waziri Mkuu amesema iwapo viongozi wa mkoa huo hawatakuwa makini katika kufanya ukaguzi kwenye vizuizi watasababisha watu wengi kuingia kiholela nchini na hivyo kuathiri mipango ya Serikali ya kuwahudumia wananchi wake.

Wakati huo huo,Waziri Mkuu amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Brigedia Jenerali Mstaafu Emanuel Maganga kufuatilia kwa umakini mwenendo wa utendaji kazi katika kizuizi cha Uvinza.

Waziri Mkuu amesema iwapo atabaini kuwepo kwa Maafisa wa kizuizi hicho wanaojiashishughulisha  na vitendo vya rushwa pamoja na kuwasumbua wananchi na abiria wanaopita kizuizini hapo awachukulie mara moja.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,


from MPEKUZI

Comments