RC Mghwira alitaka Jeshi la Polisi kujitathmini

Jeshi la Polisi Mkoani Kilimanjaro limetakiwa kujitathmini baada ya malalamiko kutoka kwa wananchi kuwa kuna baadhi ya askari polisi wanajihusisha na vitendo vya kudai rushwa.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira kwenye hafla iliyoandaliwa na Kamanda wa Polisi wa Kilimanjaro Kamishna Msaidizi wa Polisi, Hamisi Issa kwa ajili ya kufahamiana, kujenga na kuimarisha mahusiano kati ya Jeshi hilo na vyombo vingine vya umma na sekta binafsi.

Amesema kuwa vitendo hivyo vimekuwa vikichafua taswira ya Jeshi la Polisi kutokana na baadhi ya askari kutenda makosa hayo.

“Nimekuwa nikipokea malalamiko mengi kutoka kwa wananchi juu ya vitendo vya rushwa na wakati mwingine nililazimika kumueleza Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kilimanjaro Kamishna Msaidizi wa Polisi, Hamisi Issa ili  alishughulikie suala hilo,”amesema Mghwira

Hata hivyo, Julai 21, 2018, Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola ambaye anasimamia vyombo vya ulinzi nchini pia alionya vitendo vya Jeshi la Polisi kuwabambikizia wananchi makosa na kuwalazimisha kutoa rushwa huku akiwataka Watanzania watoe taarifa kwa vyombo husika kwa askari yoyote ambaye atafanya vitendo hivyo.


from MPEKUZI

Comments