Rais Magufuli Ataka Nchi zenye Uhaba wa Chakula Zije Zinunue Nchini

Rais John Magufuli ametoa wito kwa mabalozi ambao nchi zao zina uhaba wa chakula kuja kununua nchini ili wakulima wapate masoko.

Amesema hakuna haja ya kwenda kununua chakula cha wakimbizi Ulaya wakati kinapatikana Tanzania.

Rais alisema Serikali inatafuta soko la chakula ili kutowavunja moyo wakulima ambao katika msimu huu wamezalisha ziada huku nchi ikiwa na chakula cha kutosha.

Alisema hayo jana Ikulu jijini Dar es Salaam wakati wa kukabidhi hati za utambulisho za viwanja kwa mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao nchini na wawakilishi wa mashirika ya kimataifa yenye makazi yake nchini kwa ajili ya kujenga ofisi na makazi jijini Dodoma.

Jumla ya hati za utambuzi 67 zilikabidhiwa, kati ya hizo 62 ni za balozi za nchi na tano ni za mashirika ya kimataifa.

“Kama Somalia wanahitaji chakula waje wanunue hapa, kama South Sudan (Sudan Kusini) wanahitaji waje wanunue hapa, kama DRC wanahitaji waje kununua hapa,” alisema.

Rais alisema, “Kama kuna chakula kinatakiwa kupelekwa kwa refugees (wakimbizi), kwa nini mkanunue chakula kutoka nje huko Ulaya na kukisafirisha kwa gharama kubwa, si chukua hapa tu Songea.”

Rais Magufuli alisema alikutana na mkurugenzi mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), David Beasley ambaye alijionea ziada ya chakula iliyopo nchini.



from MPEKUZI

Comments