Walichokubaliana Rais Magufuli Na Mnangangwa

Rais wa Zimbabwe, Emerson Mnangagwa aliwasili Tanzania jana na kukubaliana na Rais John Magufuli kushirikiana kibiashara, utalii na kijamii.

Sambamba na hilo, kiongozi huyo alizungumzia shambulio lililofanywa dhidi yake Juni 23, katika mkutano wake wa kampeni uliofanyika mjini Bulawayo nchi humo akisema lilikuwa dogo na nchi yake iko salama.

Rais Mnangagwa alisema hayo Ikulu mjini hapa, ambapo baadhi ya wasaidizi wake na viongozi wa chama chake cha Zanu –PF walijeruhiwa.

Katika mahojiano na Shirika la Utangazaji la Uingereza, mwanasiasa huyo alilihusisha tukio hilo kufanywa na kundi la G-40 ambalo ni tiifu kwa Grace Mugabe ambaye ni mke wa Rais mstaafu, Robert Mugabe.

Mambo Matatu Waliyokubaliana
Rais Mnangagwa aliwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), saa 5:30 asubuhi na kupokewa na mwenyeji wake, Rais John Magufuli kisha kukagua gwaride la heshima na kuelekea Ikulu yalikofanyika mazungumzo.

Akizungumza na waandishi wa habari Ikulu, Rais Magufuli alisema wamezungumza jinsi ya kuimarisha uchumi wa nchi hizi mbili kiuchumi tofauti na uhusiano wa zamani uliokuwa wa kisiasa zaidi.

“Mwaka 2016 biashara kati ya Tanzania na Zimbabwe ilikuwa ni Sh18.3 bilioni sawa na Dola 8.5 milioni. Mwaka 2017 biashara ilikuwa Sh21.1 bilioni sawa na Dola za Marekani 9.5 milioni. Kuna miradi 25 ya Zimbabwe nchini yenye thamani ya Dola 32.02 milioni ,” alisema Rais Magufuli.

Alisema wamekubaliana kupitia Jumuiya ya Ushirikiano wa Nchi za Kusini mwa Afrika (Sadc) kukuza biashara.

“Ipo mikataba ya kulegeza masharti ya kibiashara katika Sadc. Baada ya uchaguzi ambao naamini atashinda tutaitumia kamati yetu maalumu kuyapitia maeneo hayo,” alisema.

“Tumekubaliana kukuza uwekezaji, nimemwambia kuna hekta 44 milioni za ardhi inayofaa kwa kilimo na kuna hekta 29 milioni zinazofaa kwa umwagiliaji. Vilevile kuna uwekezaji wa mifugo, uvuvi na uchakataji wa madini.”

Katika utalii, Rais Magufuli alisema wamekubaliana kushirikiana wakitumia wingi wa vivutio vilivyopo nchini ili kuwavutia na kutumia mikataba ya mashirika ya ndege likiwamo la Fasjet.

“Mathalan, mtalii akitoka Victoria Falls aende pia Serengeti halafu amalizie safari yake kwenye fukwe nzuri za Zanzibar,” alisema.

Rais Magufuli alisema pia wamekubaliana kuwa na ushirikiano katika huduma za jamii ikiwamo elimu, afya na utamaduni na hasa katika lugha ya Kiswahili ambayo alisema Tanzania ina walimu wa kutosha.

Rais Mnangagwa aliyewahi kuishi nchini aliishukuru Tanzania kwa kuratibu harakati za ukombozi wa Afrika.

“Dar es Salaam tuliyoishi miaka ya 1963 na 1964 ni tofauti kabisa na ya sasa. Tulijenga kambi ya kijeshi kule Bagamoyo ikiwa chini ya chama cha Frelimo tukiwa nchi ya Rhodesia (sasa Zimbabwe), Zambia na Msumbiji,” alisema.

Aliielezea Tanzania kwa Wazimbabwe kama vile mkunga wa ukombozi. Alisema hali si hivyo kwa nchi hiyo pekee bali pia kwa Namibia, Afrika Kusini na Angola, hivyo ni lazima kuishukuru.

Rais Mnangagwa alisema miaka 20 baada ya Zimbabwe kupata uhuru iliingia kwenye anguko la uchumi kutokana na kutekeleza sera ya ugawaji ardhi kwa watu weusi.

“Kwa sasa tunajitambulisha katika uwekezaji wa kimataifa. Hata zile nchi zilizojitenga baada ya kuwekewa vikwazo tunazikaribisha, lakini kwa nchi kama Tanzania ni rafiki yetu tutaendelea kushirikiana,” alisema.

Rais Mnangagwa amepanga kutembelea iliyokuwa kambi yao ya kijeshi ya Frelimo mjini Bagamoyo mkoani Pwani leo.



from MPEKUZI

Comments