ATCL: Watanzania Kaeni Mkao Wa Kukalia Kiti Cha ndege mpya ya Dreamliner 787

WATANZANIA nchini wametakiwa kukaa mkao wa kukalia kiti cha ndege mpya ya Dreamliner 787 itakayokuwa na uwezo wa kubeba abiria 262 ambayo inatarajiwa kuwasili nchini hivi karibuni.

Hayo yamesemwa jana na Ofisa wa Idara ya Biashara wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) Lily Fungamtama wakati anazungumza na wananchi waliofika kwenye banda la ATCL  lililopo kwenye Maonesho ya Biashara ya Kimataifa yanayoendelea Sabasaba jijini Dar es Salaam.

“Watanzania wakae mkao wa kukakilia kiti cha ndege mpya yenye uwezo wa kubeba abiria 262 .Ndege ambayo inauwezo wa kukaa angani muda mrefu,”alisema Fungamtama.

Aliongeza kuwa watanzania wana kila sababu ya kumuunga mkono Rais Dk.John Magufuli kwa kuhakikisha wanapanda ndege hiyo yenye uwezo wa kusafiri masafa marefu.

Amewahakikishia wananchi wote kuwa ATCL imejipanga kutoa huduma bora na za kisasa na kufafanua kuwa wafanyakazi  wa ndege zao wamepikwa katika kutoa hduma bora na kuzingatia heshima na maadili ya mtanzania.

Aliongeza kuwa wafanyakazi wa ndege wameandaliwa vema kupitia chuo cha ATCL Training Institute ambacho jukumu lake ni kuandaa wafanyakazi wenye viwango bora vya kutoa huduma katika ndege za shirika hilo.

“ATCL tunatoa huduma katika kiwango cha juu kwa kuzingatia misingi ya maadili ya mtanzania.Tumejipanga vema kuwahudumia Watanzania wote na kwa sasa tunasubiri ujuo wa ndege mpya ya Dreamliner,”alisema.

Mmoja ya wananchi waliofika kwenye banda la ATCL ambaye jina halikupatikana alisikika akisema hajapanda ndege ya Bombardier lakini atahakikisha Dreamliner 787 anaipanda.

“Hii Dreamliner lazima nitaipanda tu maana kutoka Tanzania hadi Mumbai nchini India tunasafiri angani bila kuchimba dawa.Lazima niipande tu na ni vema nikamuunga mkono Rais wangu kwa vitendo,’amesema.


from MPEKUZI

Comments