Suala la wanafunzi St. Florence waliodaiwa kudhaliliswa na mwalimu wao Laibuka Bungeni

Suala la wanafunzi waliodaiwa kudhaliliswa na mwalimu wao katika Shule ya Msingi St. Florence ya jijini Dar es Salaam limeibuka bungeni baada ya wabunge kuliombea mwongozo wa hatma ya wanafunzi hao na hatua zitakazochukuliwa.

Suala hilo limeibuka leo baada ya wabunge wawili wa Viti Maalumu wa CCM, Zainabu Vullu na Esther Mmasi kuliombea mwongozo wa Spika muda mfupi baada ya kipindi cha maswali na majibu kukamilika.

Aliyekuwa wa kwanza kuomba mwongozo ni Mbunge Mmasi ambaye alitaka kujua serikali itachukua hatua gani dhidi ya mwalimu anayetuhumiwa katika tukio hilo, Ayub Mlugu.

Baada ya kuwasilisha mwongozo huo Vullu naye aliwasilisha hoja yake akieleza jinsi tukio hilo lilivyoathiri watoto waliodaiwa kufanyiwa ukatili huo.

Akizungumzia suala hilo baada ya kuruhusiwa na Mwenyekiti wa Bunge Andrew Chenge, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama, alisema serikali imeshalijua suala hilo na italifanyia kazi na kutoa taarifa kulingana na mwenyekiti Chenge atakavyowaelekeza.


from MPEKUZI

Comments