Mahakama Yamzuia Msajili wa Vyama Kumpa Fedha za Ruzuku Profesa Lipumba

Mahakama Kuu ya Tanzania imemzuia Jaji Francis Mutungi na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya siasa nchini au Wakala wake yeyote yule kutoa fedha za ruzuku za Chama cha Wananchi (CUF), na kumpa Prof. Ibrahim Lipumba mpaka hapo mashauri ya msingi yanayoendelea Mahakamani yatakaposikilizwa.

Zuio hilo limetangazwa leo Mei 29, 2018 na Jaji Wilfred Dyansobera katika Mahakama hiyo na kusisitiza kwamba, maombi ya CUF ya kulinda fedha hizo yana nguvu za kisheria.

Taarifa za chama zinaeleza kuwa hadi amri hiyo ya Mahakama inatolewa, Jaji Mutungi na Ofisi yake ya Msajili wa Vyama imeshamruhusu Prof. Lipumba kuchukua zaidi ya shilingi Bilioni 1.5 na fedha hizo zimekuwa zikiwekwa kwenye akaunti zisizotambuliwa na Bodi Halali ya Udhamini ya chama na kisha kuhamishiwa kwenye akaunti za watu binafsi akiwemo Prof. Lipumba Mwenyewe.

Shauri kuhusu uhalali wa Bodi ya Wadhamini linaendelea kusikilizwa na inatarajiwa kuwa shahidi wa tatu wa upande wa Chama ataanza kutoa ushahidi wake mwezi Juni mwaka huu.


from MPEKUZI

Comments