Kilichosababisha Babu Tale Aachiwe Huru na Mahakama

Mkurugenzi wa kampuni ya Tip Top Connection na Meneja wa staa wa Bongo fleva Diamond Platnumz, Babu Tale ameachiwa huru  baada ya kusota rumande kwa Siku kadhaa

Tale alifikishwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar Jumatano Mei 23, 2018 kufuatia kesi yake anayodaiwa na Sheikh Hashim Mbonde kiasi cha Tsh. Milioni 250 ambapo kesi hiyo iliahirishwa baada ya hakimu aliyetoa amri ya kumkamata kutokuwepo mahakamani hapo.

Kipindi cha nyuma mahakama hiyo ilimwamuru Babu Tale alipe Sh. milioni 250 Mhadhiri wa Dini ya Kiislamu, Sheikh Hashim Mbonde, baada ya kupatikana na makosa ya ukiukwaji wa hakimiliki kwa kutumia masomo yake kibiashara bila ridhaa yake kinyume cha Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki.

 
Juzi jioni, Jaji Edson Mkasimongwa alimuachia huru kwa muda kwa kile kinachoelezwa kuwa ni makosa ya amri hiyo ya kumkamata na kumtaka afike mahakamani jana na akamwelekeza wakili wake amtaarifu wakili wa mdai afike mahakamani ili kuzisikiliza pande zote.

Hata hivyo, usikilizwaji wa hoja ambazo ziliibuliwa na mahakama yenyewe kuhusiana na amri ya kuwakamata ulikwama kutokana na upande wa mdai kutofika mahakamani.

Badala yake, Jaji Mkasimongwa aliahirisha shauri hilo hadi Juni 8, 2018 na kuagiza upande wa mdai kupewa taarifa ya wito kwa ajili usikilizwaji wa hoja zilizoibulia na mahakama yenyewe. Pia jaji alisimamisha amri ya kuwakamata hadi Juni 8.


from MPEKUZI

Comments