Wakili Albert Msando Apewa Shavu Jingine na Makonda

Wakili Albert Msando ataongoza kamati iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Paul Makonda kwa ajili ya kushughulikia kesi zote na changamoto zilizojitokeza katika zoezi la kutafuta haki za watoto waliotelekezwa na wazazi wao.

Zoezi hilo lilifungwa hapo jana April 27, 2018 ambapo wananchi 17,000 walijitokeza, kati yao 7,184 walisikilizwa, huku 270 wakipimwa DNA.

RC Makonda ameunda Kamati ya Wataalamu 15 wakiwemo Wanasheria, Maafisa Ustawi wa Jamii, Jeshi la Polisi Dawati la jinsia na Asasi za kiraia itakayofanya kazi ya kupitia mapungufu ya kisheria na Changamoto zilizojitokeza.

Kamati hiyo ambayo itaanza kazi rasmi May 05, 2018 chini ya Wakili Albert Msando ambaye ndiye Mwenyekiti wake itatoa mapendekezo kwaajili ya kufikishwa kwa mamlaka husika ili kufanyiwa maboresho.

Utakumbuka December 20, 2017 Wakili Albert Msando aliteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli katika tume itakayokuwa na jukumu la kufuatilia mali za Chama cha Mapinduzi (CCM).

Kabla ya kuteuliwa na Rais Magufuli, September 26, 2017 Wakili Msando aliteuliwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrion Mwakyembe kuwa Mjumbe wa kamati ya kupitia sheria ya Hakimiliki za kazi za wasanii.


from MPEKUZI

Comments