Mtwara: Mwanafunzi kidato cha pili ajinyonga kisa mapenzi

Binti Salma Abdalah ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha pili mkoani Mtwara aliyekuwa akiishi Mbawala Chini, amefariki dunia kwa kujinyonga, baada ya kukutwa na simu ambayo alipewa na mpenzi wake.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi mkoa wa Mtwara Lucas Mkondya, amesema tukio hilo limetokea mwanzoni mwa wiki hii baada ya wazazi wa binti huyo kuamua kumfukuza nyumbani na kumtaka kwenda kuishi kwa bibi yake kutokana na utovu wa nidhamu, na ndipo akaamua kujitoa uhai wake.

Kamanda Mkondya ameendelea kwa kueleza kwamba wazazi wake waligundua kuwa binti yao alikuwa akimiliki simu ambayo hawajamnunulia, na walipomuuliza hakuwa na jibu sahihi, ndipo baba mtu ambaye ni baba wa kufikia aliamua kumfukuza nyumbani kutokana na kuchoshwa na tabia zake za utovu wa nidhamu, na kuelekea sokoni kwenye biashara zake kumtafutia nauli, huku mama yake akielekea shambani kwenye shughuli zake za kilimo,

“Ni binti ambaye alikuwa ni mwanafunzi wa kidato cha pili, sasa asubuhi baba yake wa kufikia akasikia simu ikiita kutoka chumbani kwake, akamuambia mama yake na kumuuliza alikoipata, lakini hakuwa na jibu, baada ya hapo wazazi wake wakatoka kuelekea shambani na kumwambia kuwa wamechoshwa na tabia zake za utovu wa nidhamu hivyo wakirudi wasimkute aondoke, huku nyuma akaamua kujinyonga kwa kutumia khanga”, amesema kamanda Mkondya.

Taarifa zaidi kutoka kwa mashuhuda wa tukio wamesema binti huyo alipojinyonga aliacha ujumbe uliosema kwamba "Nampenda sana Daudi, siwezi kukaa naye mbali najua hili ni kosa kwangu lakini nawaomba wazazi wangu mumpende sana Daudi maana akiwa kwenye matatizo, mimi sitajisikia vizuri"


from MPEKUZI

Comments