Mahakama Yaamuru mmiliki wa IPTL Akatibiwe Muhimbili

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeamuru mmiliki wa IPTL, Harbinder  Sethi akatibiwe katika Hospital ya Taifa Muhimbili baada ya mshtakiwa huyo kulalamika afya yake imearibika sana.

Mbali ya Sethi, mshtakiwa mwingine ni mfanyabiashara James Rugemarila ambapo kwa pamoja wanakabiliwa na mashtaka 12 ya uhujumu uchumi, utakatisha fedha na kuisababisha Serikali hasara ya USD 22, 198,544.60 na Bilioni 309.

Mwendesha Mashtaka wa TAKUKURU, Leornad Swai amemueleza Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi leo March 28, 2018 kuwa upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na pia wanafatilia vielelezo vya upelelezi nje ya nchi.

Baada ya kueleza hayo, Seth alisimama na kumueleza Hakimu Shaidi kuwa; 'Afya yangu imearibika sana, nahitaji kupelekwa hospitali.'

Kutokana na maelezo hayo, Hakimu Shaidi amesema ni dhahiri afya ya mshtakiwa ikiangaliwa hata kwa macho inaonekana ni dhahifu.

“Naamuru mshtakiwa akatibiwe katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ili afya yake iwe njema,” amesema Hakimu Shaidi na kuahirisha kesi hiyo hadi April 11,2018.

Washtakiwa wote kwa pamoja wanakabiliwa na mashtaka 12 ya uhujumu uchumi, kutakatisha fedha na kuisababisha Serikali hasara ya Dola za kimarekani 22, 198,544.60 na Sh, bilion 309.


from MPEKUZI

Comments