Kesi ya Kutoa Lugha ya Fedheha Dhidi ya Rais Magufuli Inayomkabili Halima Mdee Yapigwa Kalenda

Kesi ya kutoa lugha ya fedheha dhidi ya Rais John Magufuli inayomkabili mbunge wa Kawe, Halima Mdee leo March 29, 2018 imeshindwa kuendelea baada ya mshtakiwa kuwa mgonjwa.

Kesi hiyo imeshindwa kuendelea katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutokana na mshtakiwa huyo kuwa nchini Afrika Kusini kwa matibabu.

Mdee anakabiliwa na shtaka moja la kutoa lugha ya matusi dhidi ya Rais,  kwa kusema, “anaongea hovyo hovyo, anatakiwa afungwe breki” kitendo ambacho kingeweza kusababisha uvunjifu wa amani.

Wakili wa Serikali, Patrick Mwita amedai hayo leo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba wakati shauri hilo lilipokuja kwa ajili ya kuendelea na ushahidi.

“Kesi hii imekuja kwa ajili ya kuendelea na ushahidi na tayari upande wa mashtaka tunaye shahidi hapa mahakamani, lakini nimepata taarifa kuwa mshtakiwa ni magonjwa na ameshindwa kufika mahakamani hapa,” -Wakili Mwita.

Baada ya kueleza hayo, wadhamini wa Mdee, Fares Robison ambaye ni Diwani wa Mbezi Juu na Martha Mtiko Diwani wa viti maalumu, wameieleza mahakama hiyo kuwa Mdee yupo Afrika Kusini kwa ajili ya matibabu. Baada ya maelezo Hakimu Simba ameahirisha kesi hiyo hadi May 3, 2018 itakapoendelea na ushahidi.


from MPEKUZI

Comments