Bavicha kula Pasaka mahabusu na kina Mbowe

Viongozi wa Baraza la Vijana Chadema (Bavicha) kesho watasherehekea Sikukuu ya Pasaka kwa kuwatembelea viongozi wa chama hicho waliopo magerezani.

Mwenyekiti wa Bavicha, Patrick Ole Sosopi ataongoza msafara wa viongozi wa baraza hilo watakaokwenda Segerea kumtembelea Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe na wenzake.

Amesema wamefikia uamuzi huo kwa lengo la kwenda kuwatia moyo na kuwa nao pamoja.

Amesema viongozi wengine watakwenda Mbeya kwa ajili ya Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi na Katibu wa Chadema, Kanda ya Nyasa, Emmanuel Masonga.

"Tunataka kusherehekea nao Pasaka na kuwafahamisha kuwa chama kinaendelea, hatuwezi kurudishwa nyuma wala kutetereshwa,"amesema.

Ole Sosopi pia amewataka vijana wa baraza hilo kuwa tayari kupambana kwa ajili ya chama.

Amesema; "Kuna mambo mengi yanaendelea na tunafahamu wazi kuna ajenda ya kutaka kukifuta Chadema, sasa nawaambia hakuna namna chama hiki kitafutwa, tupo imara na tunazidi kuimarika,'

“Vijana kazi yetu ni kulinda chama na kazi hiyo tutaifanya kwa nguvu zote bila woga, hatutaogopa kufa," amesema.


from MPEKUZI

Comments