Waziri Mkuu: Mabalozi Tafuteni Wawekezaji Wa Sekta Ya Utalii

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka mabalozi watumieni mbinu za kidiplomasia kuvutia wawekezaji katika sekta mbalimbali ikiwemo ya utalii na kutafuta masoko ya bidhaa zinazozalishwa nchini.

Pia Waziri Mkuu amewataka mabalozi hayo wakaimarishe diplomasia kwa lengo la kuzifanya nchi hizo ziendelee kushirikiana na Tanzania katika shughuli za kiuchumi na kijamii.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumamosi, Febriari 24, 2018) wakati akizungumza na Balozi Dkt. Wilbrod Slaa anayewakilisha Tanzania nchini Sweden na Balozi Muhidin Ally Mboweto anayewakilisha Tazania nchini Nigeria, katika makazi ya Waziri Mkuu, Oysterbay jijini Dar es Salaam.

Waziri Mkuu amesema Tanzania ina vivutio vingi vya utalii kama uwepo wa fukwe za bahari kuanzia Tanga hadi Mtwara, maziwa na mito, mbuga za wanyama hivyo ni vema wakajielekeza katika kuvutia wawawekezaji kwenye sekta hiyo ili Taifa lipate watalii wengi.

Amesema mbali na kutangaza sekta ya utalii, pia watafute wawekezaji kwa ajili ya kuwekeza kwenye sekta ya madini, viwanda na kutafuta masoko ili wafanyabiashara na wakulima wa Tanzania waweze kuuza bidhaa zao nje ya nchi.

“Tumejiimarisha katika mazao ya chakula na biashara, hivyo tunatakiwa kuwa na uhakika wa masoko kwenye kilimo ili mkulima anapozalisha pamba, tumbaku, kahawa, chai, korosho, dengu pamoja na mazao mengine tuwe na mahali pa kuuza, kwa hiyo washawishini wafanyabiashara kuja kununua.”

Pia Waziri Mkuu amewataka mabalozi hao wakawatambue na kuwaunganisha Watanzania waishio kwenye nchi wanazoiwakilisha ili nao washiriki kwenye ujenzi wa uchumi wa viwanda na wawasisitize wafuate sheria za nchi wanazoishi na wakumbuke nyumbani.

Waziri Mkuu amewasisitiza mabalozi hao kwenda kupunguza gharama za uendeshaji wa Balozi kwa kuzuia matumizi katika mambo yasiyo ya lazima. “Pia maslahi ya nchi lazima mkayasimamie huko muendako hasa katika masuala ya kiuchumi”

Kwa upande wao mabalozi hao  wamesema watahakikisha wanayafanyia kazi maelekezo yote waliyopewa ikiwa ni pamoja na kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na nchi wanazoziwakilisha.

(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMAMOSI, FEBRUARI 24, 2018.



from MPEKUZI

Comments