Mawakilii wa Sugu Wajipanga Kukata Rufaa

Baada ya mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi maarufu Sugu na Katibu wa Chadema Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Emmanuel Masonga kuhukumiwa kifungo cha miezi mitano jela, wakili wao Peter Kibatala amesema wanakusudia kukata rufaa.

Sugu na Masonga wamehukumiwa adhabu hiyo leo Februari 26,2018 na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Michael Mteite.

Wawili hao wamehukumiwa kwa kosa la kutumia lugha ya fedheha dhidi ya Rais John Magufuli, kosa walilotenda kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Desemba 30,2017 eneo la Uwanja wa Shule ya Msingi Mwenge jijini Mbeya.

Kibatala amesema baadaye watatoa taarifa ya nini kinaendelea ila wanakusudia kukata rufaa.

Baada ya hukumu kutolewa viongozi wa Chadema waliokuwepo mahakamani waliingia kwenye magari yao na kuelekea katika ofisi za chama hicho Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.

Wakati wa usomwaji wa hukumu hiyo, nje ya jengo la mahakama ulinzi uliimarishwa kukiwa na askari waliotanda hadi maeneo ya jirani.

Sugu ni mbunge aliyeweka rekodi ya kupata kura nyingi kuwashinda wabunge wote wa majimbo katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Katika uchaguzi huo, Sugu alipata kura 108,566 akiwaacha wapinzani wake kugawana kura 57,690.

Hukumu imetolewa na hakimu Mteite aliyesikiliza shauri hilo baada ya upande wa mashtaka na wa utetezi kukamilisha ushahidi Februari 9,2018.

Jamhuri iliwasilisha mashahidi watano na kielelezo kimoja cha sauti iliyodaiwa kurekodiwa na shahidi wa tano, Inspekta Joram Magova.

Upande wa utetezi uliwasilisha mashahidi sita wakiwamo Sugu na Masonga waliokana kutamka maneno waliyoshtakiwa kuyatoa.

Washtakiwa walitetewa na mawakili Sabina Yongo, Boniface Mwabukusi na Hekima Mwasipu kabla ya kujitoa na kazi hiyo kufanywa na Kibatala.

Kwa mara ya kwanza, Sugu na Masonga  walifikishwa mahakamani Januari 16 na kusomewa mashtaka na Wakili wa Serikali Mkuu, Joseph Pande aliyeeleza upelelezi ulikuwa umekamilika na walikuwa tayari kuendelea na usikilizaji.


from MPEKUZI

Comments