Waziri Jafo: Madarasa Ya Nyasi, Tembe, Udongo Yasitumike Katika Shule Zote Nchini

Nteghenjwa Hosseah, OR-TAMISEMI.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo amewaagiza Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi ambao kwenye maeneo yao bado kuna wanafunzi wanasomea katika madarasa ya Tembe ama yalioezekwa Nyasi au kujengwa kwa Udongo kuhakikisha wanaacha mara moja kutumia madarsa hayo na kujenga madarasa bora.

Waziri Jafo ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya nne ya Uongozi wa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi yanayotolewa kupitia ofisi ya Rais Tamisemi kwa kushirikiana na Taasisi ya Uongozi yenye lengo la kujenga uwezo wa viongozi kuweza kutawala kwa ufanisi.

“Viongozi wangu nataka Mkakusanye mapato ya ndani kwa nguvu zote na Fedha hizo mzitumie kwenye miradi ya maendeleo na kwa wale ambao mpaka leo wanafunzi wanasomea kwenye mazingira duni hawana madarasa bora watoto wanasomea kwenye madarsa ya Tembe, mengine yameezekwa kwa Nyasi nahitaji muelekeze Nguvu katika ujenzi wa madarasa bora na hayo ya Tembe yotoweke kabisa; Mjenge madarasa ambayo wanafunzi watajiskia fahari kusoma”Alisema Waziri Jafo.

Waziri Jafo hakusita kuwakumbusha Viongozi  kuhusu Usimamizi wa Ujenzi wa Miundombinu ya Afya 212 vinavyoendelea kujengwa hivi sasa katika ameneo yote yote Nchini.

Niwapongeze baadhi ya Wakurugenzi ambao mpaka sasa wamefanya kazi nzuri sana ya Usimamizi wa ujenzi wa Miundombinu hiyo ya Afya wameshakamilisha ujenzi na wamejenga mpaka Njia za kutembelea(Walk Way) katika vituo hivyo na nataka mpaka Tarehe 30 April 2018 Kila Halmashauri iliyopokea Fedha za ujenzi wa Miundombinu ya Afya iwe imekamilika.

Waziri Jafo alitumia nafasi hiyo pia kuwakumbusha viongozi mara wapatapo mafunzo haya kuheshimu  mipaka yao ya kazi, kuboresha mahusiano kazini, kutunza Siri za Serikali na kusimamia Maadili katika maeneo ya kazi.

Awali akizungumza katika Ufunguzi wa  Mafunzo ya Uongozi Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi Prof. Joseph Semboja amesema kuwa mafunzo haya yanakamilisha mtiririko wa mafunzo yaliyofunguliwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa  Tanzania Mhe. Majaliwa K. Majaliwa miezi nane iliyopita na baada ya mafunzo haya yanayoanza leo tutakuwa tumewafikia   Viongozi 324.

Prof.Semboja aliongeza kuwa Lengo la mafunzo haya ni yale yale ambayo ambayo yamelengwa tangu Kikao cha Mwanzo cha Mafunzo haya ambayo ni kuimarisha uwezo wa kufanya maamuzi wa Kimkakati  kwa kuzingatia mahitaji ya jamii kwa manufaa mapana ya sasa nay a baade ya Jamii Tunayoihudumia.

Sambamba na hilo Mkutano huu pia unalenga kuongeza uwezo wa Viongozi wetu katika kuongoza watu na rasillimali zingine zilizoko kwenye maeneo yetu ili kwa pamoja tuweze kufikia malengo ya pamoja.

Alisisitiza kuwa Mafunzo haya yatajielekeza katika Kuimarisha Sifa Binafsi za Viongozi  kwa sababu Viongozi ndio wanaowasimamia wananchi katika kiLA Eneo hivyo ni lazima kila kiongozi aweze kujitenegenezea Sifa binafsi ili akubalike na kuhesimika katika Jamii husika.

“Sifa hizi binafsi tunazozizungumzia ni Ushawishi, Kuaminika, Uadilifu, Mtenda Haki, Muumini wa Utawala bora na Utawala wa Sheria na zaidi kuwa mchahapa kazi na awe na weledi wa hali ya juu sasa haya yote yatafundishwa kupitia mafunzo haya ya namna gani Kiongozi anaweza Kujijengea Sifa Binafsi katika Jamii tunazoziongoza.

Akitoa Neno la Shukrani kwa niaba ya viongozi walioshiriki katika Mafunzo haya Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Mhe. Joseph Mkirikiti ameshukuru OR-TAMISEMI na Taasisi ya Uongozi kwa kuandaa mafunzo haya na zaidi ameahidi Umakini wa washiriki kwa siku zote za mafunzo.

Mafunzo haya ya awamu ya Nne na ya mwisho kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa imegususa Viongozi kutoka katika Mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani, Tanga, Kilimanjaro na Arusha.


from MPEKUZI

Comments