Mwalimu Atiwa Mbaroni Kwa Lugha Ya Matusi Mtandaoni

JESHI  la Polisi Mkoa wa Mwanza linamshikilia Mwalimu wa Shule ya Sekondari  Mkolani, Deogratius Kisandu, akidaiwa kutumia lugha ya matusi, kejeli na kudhalilisha katika ukurasa wake wa Facebook.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi, alisema  Kisandu alikamatwa jana baada ya kuwapo taarifa kuhusu kuonekana ujumbe wa matusi na lugha zisizofaa  katika ukurasa  wake ya Facebook.

Alisema walimfuatilia mtuhumiwa na kumkamata akiwa na simu yake ambayo huitumia kupeleka na kuandika matusi hayo kinyume na Sheria Namba 4 ya Makosa ya Mtandao ya Mwaka 2015.

“Polisi bado wanaendelea na  na mahojiano na upelelezi dhidi ya mtuhumiwa. Utakapokamilika atafikishwa mahakamani kwa mujibu wa sheria.

“Taarifa zinaonyesha kuwa mtuhumiwa amewahi kushtakiwa kwa makosa kama hayo kipindi cha nyuma,” alisema Kamanda Msangi.

Kamanda   amewataka  vijana wanaotumia mitandao ya  jamii kuacha kwa sababu  ni kosa kwa mujibu wa Sheria ya Makosa ya Mtandao ya Mwaka 2015.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella, alisema alipokea  malalamiko kutoka kwa wananchi siku mbili zilizopita kuhusu lugha ya kudhalilisha, matusi na kejeli  inayotumiwa na Kisandu ambaye pia ni mtumishi wa umma, katika  ukurasa wake wa Facebook.

“Tumetumia siku mbili mpaka kumpata Kisandu. Mwanzoni nilifikiri labda haya mambo yanafanywa na mtu ambaye si raia wa Tanzania lakini katika mahojiano amekiri yeye ni Mtanzania.

“Kwa kweli lugha anayoitumia ni ya kudhalilisha, matusi na kejeli na haifai kutumiwa kutokana na utamaduni wetu,” alisema.

Meneja wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Kanda ya Ziwa,   Lawi Odiero, alisema sheria ipo na inakataza matumizi mabaya ya mitandao na  kwa kuwa kesi hiyo ipo polisi  atatoa ushirikiano unaohitajika kusaidia uchunguzi.


from MPEKUZI

Comments