Mbunge aliyesimamia kiapo cha Raila Odinga Akamatwa

Mbunge wa Ruaraka Tom J Kajwang’, ambaye alisimamia “kuapishwa” kwa kiongozi wa muungano wa Nasa Raila Odinga kwenye viwanja vya Uhuru Park Jumanne amekamatwa.

Mbunge huyo amekamatwa leo Jumatano mchana na maofisa wa polisi ambao hawakuwa wamevalia sare nje ya Mahakama ya Milimani jijini Nairobi.

Alikamatwa muda mfupi baada ya kuhudhuria katika Mahakama Kuu mbele ya Jaji George Odunga kusikiliza uamuzi wa kesi aliyowawakilisha wabunge wanaopinga kukatwa mishahara yao na posho.

Kajwang’ na mwanasheria mwingine Miguna Miguna, ndio walikuwa wasimamizi wakuu wa matukio ya kwenye viwanja vya Uhuru Park yaliyomalizikia kwa “kuapishwa” Odinga kama ‘rais wa watu’.

Wakati wa sherehe za kiapo Kajwang’ alikuwa amevaa vazi na wigi na alishangiliwa sana na wafuasi wa Nasa.

Odinga alikula “kiapo” huku Kajwang’ akiwa amesimama nyuma yake japokuwa wajibu wake katika tukio hilo bado haujafahamika.


from MPEKUZI

Comments