Mkuu wa jeshi Algeria afariki kutokana na mshtuko wa moyo

Mkuu wa jeshi nchini Algeria Gaid Salah, ambaye pia alikuwa mwenye ushawishi mkubwa katika siasa za nchi hiyo zilizokabiliwa na misukosuko mwaka huu, amefariki dunia. 

Rais mpya wa Algeria Abdelmadjid Tebboune ametangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa na siku saba kwa jeshi kuhusiana na kifo cha ghafla cha Salah aliyekuwa na umri wa miaka 80. 

Shirika la habari la serikali APS limeripoti kuwa alipatwa na mshtuko wa moyo akiwa nyumbani na kisha akakimbizwa hospitali ya kijeshi. 

Salah alionekana kuwa na ushawishi mkubwa katika kujiuzulu kwa rais Abdelaziz Bouteflika mwezi Aprili, akiongeza mbinyo kwa kiongozi huyo wa muda mrefu baada ya maandamano ya umma nchini humo. 

Katika miezi iliyofuata, Salah alikaidi masharti ya waandamanaji kuwa pia naye ajiuzulu. 

Aliunga mkono uchaguzi ulioandaliwa mwezi huu, ambao ulimuweka madarakani Abdelmadjid Tebboune.


from MPEKUZI

Comments