Waziri Mkuu: Serikali Imedhamiria Kuboresha Huduma Za Afya

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali imedhamiria kuboresha huduma za afya kwenye maeneo mbalimbali nchini yakiwemo ya halmashauri ya wilaya ya Lushoto.

Amesema lengo ni kuhakikisha kila kata inakuwa na kituo cha afya chenye uwezo wa kutoa huduma mbalimbali muhimu zikiwemo za maabara, upasuaji na mama na mtoto.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumatano, Oktoba 31, 2018) wakati akizungumza na wakananchi katika kata ya Malindi, baada ya kutembelea jengo la soko mbogamboga la Malindi.

Waziri Mkuu amesema Serikali imejipanga vizuri katika sekta ya afya baada ya bajeti ya kununulia dawa kuongezeka kutoka sh. bilioni 31 kwa mwaka na kufikia bilioni 269.

“Hatutaki tena kusikia mgonjwa anaenda hospitali na kukosa dawa biashara hiyo tumeimaliza, Rais Dkt. John Magufuli ametoa fedha nyingi kwa ajili ya ununuzi wa dawa.”

Amesema katika wilaya ya Lushoto Serikali imetenga sh. bilioni 1.4 kwa ajili ujenzi na ukarabati wa majengo ya vituo vya afya vya kata za Kangagai. Mnazi na Mlola.

“Halmashauri wekeni mpango thabiti wa kujenga wodi mbili kati yake moja ya wanaume na nyingine ya wanawake, lengo la Serikali ni kuboresha huduma za afya kwa wananchi.”

Aizungumzia kuhusu mradi wa ujenzi wa soko, Waziri Mkuu amesema mradi huo ni sehemu ya huduma zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya kuboresha huduma za jamii nchini.

Waziri Mkuu ametaja huduma nyingine zinazotolewa na Serikali kwa wananchi ni za afya, elimu, maji, uchumi na ujenzi na uboreshwaji miundombinu mbalimbali ikiwemo ya barabara.

Hivyo, amewataka wananchi watumie vizuri soko hilo  ambalo linatoa fursa kwao kufanya biashara katika eneo zuri na kuwawezesha kuuza bidhaa zao zikiwa katika ubora.

Pia amewashauri wakulima hao wajiunge katika vikundi na kuanzisha ushirika wao ili waweze kusaidiwa na Serikali katika kupata mikopo kwa ajili ya kuzalisha kwa ubora zaidi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Lushoto, Bibi Ikupa Mwasyoge amesema kukamilika kwa soko hilo kutainufaisha halmashauri na wananchi.

Bibi. Ikupa amesema ujenzi wa jengo hilo la soko la ghorofa mbili lililojengwa kwa awamu mbili ulianza mwaka 2011 na umekamilika Septemba 2018, umegharimu sh. bilioni 1.1.

Amesema halmashauri itanufaika kwa kupata ushuru na wananchi ambao wengi wao ni wakulima wa mboga na matunda watakuwa na sehemu ya uhakika wa kufanyia biashara.

“Wakulima 35,000 wa kata ya Malindi na kata jirani za Lukozi, Manolo na Shume wanaozalisha wastani wa tani 5,900 za mboga na matunda kwa mwaka watanufaika.”

Naye, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema Serikali imefanya kazi kubwa katika kuboresha huduma za afya nchini.

Amesema bajeti ya dawa katika halmashauri hiyo imeongezeka kutoka sh milioni 183 za dawa zilizokuwa zinatolewa awani na sasa imefikia sh milioni 565.

Mbunge wa jimbo la Mlalo, Bw. Rashid Shangazi ametumia fursa hiyo kuishukuru Serikali kwa kuwasaidia wananchi wa halmashauri kuongeza thamani ya mazao yao kabla ya kuuza.

Awali,Waziri Mkuu alizindua jengo la utawala la Halmashauri ya wilaya ya Lushoto lililogharimu sh. bilioni 4.3. Kukamilika kwa jengo hilo kutaboresha huduma kwa wananchi.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMATANO, OKTOBA 31, 2018.


from MPEKUZI

Comments