Zitto Kabwe : Fedha za Korosho ni za wakulima

Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo) Kabwe Zitto amesema kitendo cha Serikali kutaka kuchukua asilimia  65 za ushuru wa mauzo ya korosho nje ya nchi si sahihi kwa sababu fedha hizo ni za wakulima.

Kiongozi  huyo wa ACT-Wazalendo pia amezungumzia uamuzi wa Serikali kutaka  kuanzisha Akaunti Jumuifu ya Hazina (TSA), akibainisha kuwa  ni uvunjifu wa Katiba na Sheria za  ukaguzi.

Zitto ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Juni 28, 2018 bungeni mjini Dodoma katika mjadala wa Sheria ya Fedha ya mwaka 2018.

“Hakuna zao lolote lenye ushuru wa mauzo nje zaidi ya Korosho, hili linatakiwa kueleweka kwanini iwe korosho,” amesema.

Amesema utaratibu uliopo sasa kuhusu korosho ulianzishwa na wadau wenyewe wa zao hilo, si Serikali na kwamba lengo ni kuboresha zao hilo baada ya kutambua Serikali haina fedha.

Zitto amesema mwanzo walianza kwa kukubaliana kukatwa  asilimia tatu na sasa imefikia asilimia 65 ili asilimia 35 ziiende serikalini.

“Fedha hizo asilimia 65 ni za wakulima na si za Serikali kama anavyosema AG (Dk Adelardus Kilangi-Mwanasheria Mkuu wa Serikali),” amesema.

Baada ya maelezo hayo, Spika Job Ndugao alimhoji Zitto kama Mfuko wa Korosho haukuwa mali ya umma kwanini makusanyo yake yafanywe na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Akijibu swali hilo, Zitto amesema, “wadau walisema kati ya asilimia 100, asilimia 35 zitakuwa zinakwenda TRA kama malipo ya kuwakusanyia fedha kwa hiyo mheshimiwa spika hizi asilimia 65 ni za kwao kuzichukua fedha hizi haiwezekani. Tusiwe  wakatili jamani kwa mambo ambayo wameomba wenyewe watozwe.”

Kuhusu uanzishwaji wa akaunti ya TSA, Zitto amesema inakiuka sheria ya ukaguzi wa Taifa kwa kumpa mamlaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kukaguza akaunti hiyo.

“Lakini ni kinyume cha Katiba ya nchi naliomba Bunge  kutokuwa sehemu ya uvunjifu huu wa sheria na Katiba,” amesema.


from MPEKUZI

Comments