Uchaguzi CHADEMA: Heche Asema Kura Hazikutosha, Matiko Aomba Ushirikiano

Mbunge wa Tarime Vijijini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), John Heche, amewashukuru wanachama wenzake waliompigia kura ijapokuwa hazikumpa ushindi, katika kinyang'anyiro cha kumtafuta Mwenyekiti wa Kanda ya Serengeti, uchaguzi uliofanyika usiku wa kuamkia leo Desemba 2,

Katika uchaguzi huo wa ndani Mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko, aliibuka mshindi kwa kupata kura 44 dhidi ya kura 38 alizopata Mbunge Heche na kumfanya Matiko kuwa Mwenyekiti wa Kanda hiyo.

"Nawashukuru sana wanachama wenzangu na wajumbe kwa kura mlizonipa japo hazikutosha, nawapongeza wengine wote waliotumia Demokrasia yao kuchagua wagombea wenzangu, nawatakia kila la kheri walioshinda katika majukumu magumu mbele yetu" ameandika Mbunge Heche.

Kwa upande wake  Ester Matiko ambaye pia ni mbunge wa Tarime mjini amesema kura alizopata zinaonyesha imani kwake na kuahidi kufanya kila lililo ndani ya uwezo wake kuijenga Chadema katika kanda hiyo.

Matiko aliwaambia wajumbe wa mkutano huo wa uchaguzi uliosimamiwa na Meya wa Ubungo, Boniface Jacob kuwa umoja na ushirikiano miongoni mwa viongozi, wanachama na wananchi ndiyo siri ya mafanikio na kuwaomba wagombea wote kuvunja makambi kwa sababu baada ya uchaguzi kambi inayosalia ni ya Chadema.


Heche ambaye pia ni mbunge wa Tarime vijijini ndiye alikuwa mwenyekiti wa kanda hiyo tangu mwaka 2014.


from MPEKUZI

Comments