Waziri Jafo Atengua Maamuzi Yote.......Kaagiza Wagombea Wote Waliongeliwa Uchaguzi Serikali za Mitaa Warudishwe

Waziri wa Nchi ofisi ya Rais TAMISEMI Mhe. Selemani Jafo ametangaza kuwaruhusu wagombea wote waliochukuwa fomu na kuzirejesha kwa ajili ya kugombea nafasi mbalimbali katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika nchini Tanzania Novemba 24, 2019 na amefuta maamuzi yote yaliyofanywa na wasimamizi wa uchaguzi Nchini kote ya kuwaengua wagombea wa vyama mbalimbali. 

Waziri Jafo ametoa uamuzi huu  leo November 10, 2019 jijini Dodoma alipokuwa akizungumza na wanahabari leo

“Natoa Muongozo Wagombea wote waliochukuwa fomu na kuzirejesha waruhusiwe kushiriki uchaguzi huo, waingie ulingoni, hakuna kutafuta sababu, labda kama sio Raia wa Tanzania, hajajiandikisha Kwenye Mtaa husika, amejiandikisha mara mbili au hajadhaminiwa na Chama chake

“Wote waliochukua na kurejesha fomu wanaingia ulingoni na ratiba za kampeni zitaanza kupokelewa, hakuna kuweka mpira kwapani, hakuna kuruka kenchi,hakuna kukimbiana wote watashiriki Uchaguzi huu wa Serikali za Mitaa, hakuna kutafuta visingizio tena

“Kwahiyo nafuta maamuzi yaliyofanywa na Wasimamizi wa Uchaguzi Nchini kote ya kuwaengua Wagombea wa Vyama mbalimbali, tunafanya hivi Kwa busara, tusijiangalie sisi kama Viongozi wa Vyama mbalimbali, tuangalie watu ambao wapo kule chini wanataka kushiriki uchaguzi huu

“CHADEMA na ACT walitangaza kujiondoa, cha ajabu mpaka jana kuna Wanachama wa Vyama hivyo bado walikuwa wanaendelea kupeleka fomu, kwa hiyo licha ya utashi wa Viongozi, kule site hali ni tofauti watu wanataka kushiriki uchaguzi ndo maana nimetoa muongozo huu wa kuwaruhusu” Amesema Waziri Jafo


from MPEKUZI

Comments