Mawaziri Wa Mambo Ya Nje Wa Nchi NORDIC Na Afrika Watembelea Mradi Wa SGR

Mawaziri wa Mambo ya nje kutoka nchi za Nordic na Afrika watembelea Mradi wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa – SGR kipande cha Dar es Salaam – Morogoro, kuanzia Stesheni ya Dar es Salaam hadi Vingunguti jijini Dar es Salaam Novemba 09, 2019.

Lengo la ziara hiyo ni kuona hatua kubwa ambayo serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepiga katika kuboresha miundombinu ya usafirishaji ukizingatia miundombinu ni moja kati ya vitu muhimu katika kuimarisha uhusiano na ushirikiano baina ya nchi za Nordic na Afrika.

Mawaziri hao walipata fursa ya kuona maendeleo ya ujenzi wa stesheni ya reli ya kisasa inayojengwa eneo la stesheni jijini Dar es Salaam, daraja la treni lenye urefu wa KM 2.5 pamoja na maendeleo ya Mradi kwa ujumla kipande cha Dar es Salaam – Morogoro ambao umefikia zaidi ya 70%.

Miongoni mwa Mawaziri waliopata fursa ya kutembelea mradi ni kutoka nchini Egypt, Nigeria, Angola pamoja na Niger. Ziara hii ni matunda ya mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya nje kutoka nchi za Nordic na Afrika uliojadili mambo kadhaa kuhusu kuboresha uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya nchi za Afrika na nchi za Nordic uliofanyika katika ukumbi wa kimataifa wa mikutano wa Mwl. J.K Nyerere jijini Dar es salaam.

Aidha Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania Ndugu Masanja Kungu Kadogosa amewashukuru Mawaziri hao kwa kuchagu kutembelea mradi wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa kwa kuwa ipo Miradi mingi ya kimkakati.

Naye Waziri wa Mambo ya Nje nchini Nigeria Mhe. Zubairu Dada amesema kuwa amefurahishwa na emeipongeza Tanzania kwa kutumia fedha zake za ndani kujenga reli ya kiwango cha kimataifa kuanzia Dar es Salaam hadi Makutupora Singida. Ameongeza kuwa Afrika haiwezi kuendelea kusubiri maendeleo hivyo jitihada za haraka zinatakiwa kufanywa ili kuhakikisha miradi ya miundominu inakamilika haraka ili watu wapate huduma.


from MPEKUZI

Comments