Evans Aveva, Kaburu, Hans Pope Kuanza Kujitetea Novemba 20

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, imesema vigogo wa Klabu ya Simba akiwamo Rais wa zamani, Evans Aveva na wenzake wawili wanaokabiliwa na tuhuma za kughushi na matumizi mabaya ya madaraka, wataanza kujitetea Novemba 20, mwaka huu.

Kesi hiyo ilipangwa kwa ajili ya kutajwa jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, ambapo Wakili wa Serikali, Sylvia Mitanto, aliomba tarehe nyingine ya kusikilizwa.

Hata hivyo, Hakimu Simba alihoji kwanini kesi ilikuja kwa ajili ya kutajwa wakati ilipangwa kwa kusikilizwa?

Wakili Mitanto alidai tarehe iliyopita waliitaarifu mahakama kuwa wamekata rufani kupinga uamuzi wa mahakama hiyo kuwaona washtakiwa hawana kesi ya kujibu katika Mashtaka ya kutakatisha fedha, na kwamba wanaomba tarehe nyingine kusubiri uamuzi wa rufani.

Hakimu Simba alisema mahakama hiyo itapanga tarehe ya kusikilizwa kwa utetezi na kama kutakuwa na masuala ya rufani waijulishe mahakama.

Baada ya kueleza hayo, Hakimu Simba alisema itaanza kusikilizwa utetezi wa washtakiwa Novemba 20, mwaka huu.

Mbali na Aveva, washitakiwa wengine ni aliyekuwa makamu wa rais, Geofrey Nyange maarufu Kaburu na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili, Zacharia Hansppope wamekutwa na kesi ya kujibu katika mashtaka saba na kuondolewa mashtaka mawili ya utakatishaji fedha.


from MPEKUZI

Comments