Waziri Simbachawene Aagiza Waliokiuka Maagizo Ya Serikali Wafutiwe Vibali Vya Kuingiza Na Kusafirisha Vyuma Chakavu.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mh. George Simbachawene ameagiza kufutwa kwa vibali vya wafanyabiashara wote wanaosafirsha vyuma chakavu ambao hawakufuata maelekezo na maagizo ya Serikali.
 
Amesema hayo jijini Dodoma wakati wa mkutano wa kupokea ripoti ya kamati aliyoiunda kwa ajili ya uchunguzi wa makontena ya bidhaa za chuma chakavu yaliyokua yamekamatwa  kwa uchunguzi katika bandari ya jiji la Dar Es Salaam. Ninaagiza wafanyabiashara wote waliokiuka maagizo na maelekezo ya Serikali wafutiwe vibali vyao.
 
Waziri Simbachawene ameipongeza kamati hiyo kwa kazi nzuri waliyoifanya na amepokea mapendekezo yote yaliyopendekezwa na kamati hiyo. “Nawapongeza sana mmefanya kazi kubwa na mapendekezo yote yaliyotolewa na Kamati nimeyapokea na ninaagiza NEMC kama msimamizi mkuu kusimamia jambo hili’ alisema Waziri
 
Aliongeza kuwa Wafanyabiashara wa vyuma chakavu siyo wakweli mana wengi wanasafirisha bidhaa zingine tofauti na vyuma chakavu huku wakisingizia kuwa wamebeba vyuma chakavu wakati siyo kweli.  Vitu mbalimbali vinasafirishwa kama vile mifuniko ya chemba, injini za vifaa vya moto, mita za maji, vipande vya bomba na vingine ni vipya kabisa na haviko kwenye kundi la vyuma chakavu.
 
Akiongea wakati wa kumkaribisha Mh. Waziri, Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la usimamizi wa hifadhi ya mazingira (NEMC)  Dkt Gwamaka Mafwenga alisema kuwa ziko Kampuni sita ambazo makontena yao yalikamatwa Bandarini  na yalikua yakifanyiwa uchunguzi. Makampuni hayo ni J. M Kambi and General Services(makontena 88), JBR Group of Companies(makontena 35), Villa Plast L.td(makontena 3) , Three Star Metal Group(makontena 12) na Steel Com Ltd(makontena 2).
 
  Waziri Simbachawene alifanya ukaguzi katika bandari ya Dar Es salaam na kuagiza makontena yote ya Kampuni tajwa hapo juu yaliyokua yamebeba shehena ya vyuma chakavu kuzuiliwa kusafirisha bidhaa hizo na kufanyike uchunguzi wa haraka sana juu ya makontena hayo.





from MPEKUZI

Comments