Waziri Lugola Afanya Mazungumzo Na Balozi Wa Ethiopia Nchini, Jijini Dodoma Leo

Na Felix Mwagara, MOHA, Dodoma.
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amefanya mazungumzo na Balozi wa Ethiopia nchini, Yonas Yosef Sanbe na kumuhakikishia ushirikiano zaidi kati ya Wizara yake na Ubalozi huo nchini.

Mazungumzo hayo ya zaidi ya saa moja yalifanyika ofisini kwa Waziri Lugola, jijini Dodoma, leo, ambayo yalijadili masuala mbalimbali ikiwemo uimarishaji wa ushirikiano kati ya Tanzania na Ethiopia.

Waziri Lugola alimuhakikishia Balozi huyo kuwa, Tanzania itaendelea kuwa salama kwa kuwa Wizara yake imejipanga vizuri kuendelea kuwalinda raia na mali zao pamoja na wageni wote waishio nchini.

“Mheshimiwa Balozi nashukuru sana kwa kunitembelea, najisikia furaha kwa ujio wako na karibu sana wakati wowote, Wizara pamoja na nchi yangu kwa ujumla tutaendelea kushirikiana nanyi katika masuala mbalimbali,” alisema Lugola.

Kwa upande wake Balozi Sanbe, alimshukuru Waziri Lugola kwa mazungumzo waliyoyafanya na kumuhakikishia ushirikiano zaidi kati ya Ethiopia na Tanzania.


from MPEKUZI

Comments