Serikali ya Tanzania na Barrick waunda Kampuni Mpya ya Kusimamia Madini inayochukua nafasi ya Kampuni ya Acacia.

Jitihada za Rais John Magufuli za kuhakikisha rasilimali za Tanzania zinalindwa, zimeanza kuzaa matunda baada ya serikali na Kampuni ya Barrick Gold Corporation kuingia ubia na kuanzisha kampuni mpya ya Twiga Mining Co. Ltd inayochukua nafasi ya Kampuni ya Acacia.

Kampuni ya Twiga iliyosajiliwa nchini na makao yake makuu yatakuwa Mwanza, Serikali ya Tanzania itamiliki asilimia 16 na Barrick Gold Corporation itakuwa na asilimia 84.

Sasa ndio itakayosimamia migodi mitatu iliyokuwa inasimamiwa na Acacia ambayo ni Bulyanhulu, Buzwagi na North Mara na itaendesha shughuli zake zote nchini.

Hatua hiyo, imekuja baada ya Kampuni ya Barrick kuizika rasmi Acacia na kufunga ofisi zake zilizokuwepo jijini London, na kufuta kesi na madeni yote ambayo kampuni hiyo ya Acacia iliyafungua dhidi ya serikali.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa Palamagamba Kabudi alisema hatua hiyo imeingiza Tanzania katika historia mpya ya ukombozi wa kiuchumi.

Alisema kuanzishwa kwa kampuni hiyo mpya sasa kumefuta migogoro yeyote iliyokuwepo baina ya serikali na Acacia ambayo hisa zake za asilimia 63.9 zote zilinunuliwa na hivyo kumilikiwa na Barrick Gold Corporation.

Alieleza kuwa pamoja na kufuta migogoro hiyo, pia wamekubaliana kuwa Barrick itailipa Tanzania kiasi cha dola za Marekani milioni 300 kwa ajili malipo ya kodi zote zilizokuwa haijalipwa na migogoro mingine.


from MPEKUZI

Comments