Aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto Ahojiwa TAKUKURU Kwa Ubadhirifu wa Milioni 300

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa - Takukuru Mkoa wa Tanga inamhoji aliyekuwa mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Lushoto Kazimbaya Makwega kwa tuhuma za ubadhirifu wa Shilingi 300 milioni za upimaji wa viwanja katika shamba la Mnazi wilayani Lushoto.

Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Tanga, Christopher Mariba jana alisema Makwega alihamishiwa Halmashauri ya Wilaya Mbozi kabla kutenguliwa na Rais John Magufuli.

Alisema zipo fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya upimaji wa viwanja na mkataba ulikuwa wa Sh300 milioni ambapo mtuhumiwa kwa kutumia nafasi yake anatuhumiwa kubadilisha baadhi ya vipengele.

Alivitaja vipengele vinavyodaiwa kubadilishwa mkurugenzi huyo ni vile vilivyoitaka Kampuni ya Geoplan (EA) ya jijini Dar es Salaam kuweka kiasi cha gharama kwa ajili ya tahadhari ikiwa itachelewa kukamilisha kazi ile gharama itakatwa.

Kamanda huyo wa Takukuru alisema mkataba huo wa upimaji ulitakiwa uanze Juni  28 mwaka 2013 hadi Agosti 28, 2018 kitu ambacho hakikufanyika hadi Desemba 3, 2018 ambapo muda ulikuwa  kinyume na taratibu za mkataba na hata fedha za dharura zilizotakiwa kukatwa kama kipengele cha 44 kinavyoonyesha hazikukatwa.


from MPEKUZI

Comments