TFF Wamjibu Waziri Mwakyembe

Shirikisho la Soka nchini (TFF), limejibu alichohoji Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe utaratibu upi ulitumika wakati wa kumsimamisha kazi alyekuwa Kocha wa Taifa Stars, Emmanuel Amunike na kutaka apatiwe majibu.

Mwakyembe pia alihoji mikakati ya TFF ya kuhakikisha soka la Tanzania linakuwa baada ya kumfuta kazi Amunike ama la wajiuzulu kuwapishe wengine katika nafasi zao.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Julai 11, na TFF kupitia kwa Katibu Mkuu wake, Kidao Wilfred imesema itatoa taarifa kamili kuhusiana na makubaliano hayo ya kusitisha mkataba baada ya maamuzi hayo yaliyotokana na mazungumzo ya msingi baina ya TFF na Amunike.

Aidha ikijibu kile alichodai Waziri Mwakyembe kuwa ni dharau za viongozi wa soka hapa nchini baada ya viongozi wa TFF kuitwa katika kikao na kutokufika badala yake wakatuma wasaidizi, taarifa hiyo imesema viongozi wa shirikisho hilo kwa maana ya Rais, Makamu wa Rais na Katibu Mkuu walishindwa kuhudhuria kutokana na kubanwa na majukumu mengine ya kikazi.

“Tulitoa taarifa kwa wasaidizi wa Mh Waziri kuwa Katibu Mkuu wa TFF atakuwa na ratiba ya mapokezi na kazi kwa wakaguzi kutoka FIFA kwa ajili ya ukaguzi wa fedha za FIFA kwa mwaka 2018, ratiba ambayo tayari ilikwishapangwa kwa pamoja tangu Januari Mosi mwaka huu.

“Pia tuliwajulisha kuwa Rais Wallace Karia yupo nje ya nchi na Makamu wa Rais Athuman Nyamlani atakuwa na kikao cha makubaliano na uongozi wa Fountain Gate Academy kuhusiana na timu zetu za taifa za Vijana.

“TFF imekuwa na vikao vya mara kwa mara na Mh Waziri mwenye dhamana ya Michezo kujadiliana kuhusiana na masuala mbalimbali yahusuyo mpira wa miguu na tumekuwa tukishiriki bila kukosa hata pale tulipopata taarifa za dharura katika muda wa jioni na kutakiwa kuhudhuria kikao Dodoma asubuhi inayofuata na tunasafiri usiku kuwahi vikao hivyo,” imesema taarifa hiyo.


from MPEKUZI

Comments