Huawei na mashirika yake mengine 70 yawekwa katika orodha nyeusi ya Marekani

Wizara ya Biashara ya Marekani imetangaza kuliweka Shirika la Huawei pamoja na mashirika mengine yapatayo 70 yanayofungamana nalo katika orodha yake nyeusi.

Hatua hiyo iliyotangazwa na wizara hiyo ya Marekani inasema kwamba baada ya hapo shirika hilo litazuiwa kununua vifaa kutoka kwa mashirika ya Kimarekani isipokuwa baada ya kupata idhini ya serikali ya Washington. 

Wizara ya Biashara ya Marekani imedai kwamba, kuna ushahidi unaoifanya Washington kuamini kwamba shughuli za shirika hilo, zinakiuka usalama wa taifa wa nchi hiyo. 

Aidha viongozi wa Marekani wamedai kwamba uamuzi huo utapelekea kuwa magumu mauzo ya baadhi ya bidhaa zinazozalishwa na Huawei ndani ya Marekani au kulifanya jambo hilo kutowezekana kabisa. 

Jumatano ya jana Rais Donald Trump wa Marekani alitia saini sheria ambayo inapiga marufuku vifaa vya mawasiliano vilivyotengenezwa na mashirika ambayo yanahatarisha usalama wa taifa wa Marekani.
 
Tayari shirika hilo limetoa taarifa ya kulaani hatua hiyo ya Marekani na kuongeza kwamba, uamuzi huo wa Washington unakiuka sheria za kimataifa. 

Serikali ya Trump na kwa visingizio tofauti vikiwemo vitisho vya kiusalama, imekuwa ikishadidisha mashinikizo dhidi ya washirika wake likiwemo Shirika la Huawei ambalo ni shirika kubwa la mawasiliano la China kuuza bidhaa zake ndani ya taifa hilo. 

Hii ni katika hali ambayo Mike Pompeo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani amedai kwamba shirika hilo la mawasiliano la Huawei linaisaidia serikali ya Beijing kufanya ujasusi.


from MPEKUZI

Comments