Waziri Mkuu Azindua Mradi Wa Ujenzi Wa Kituo Cha Afya Koromije

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amefungua mradi wa ujenzi na ukarabati mkubwa wa kituo cha afya cha kata ya Koromije wilayani Misungwi na amewahakikishia wananchi kuwa Serikali imejipanga vizuri kuboresha huduma za afya.

Amesema uboreshaji huo unahusisha ujenzi wa chumba cha upasuaji, maabara, chumba cha kujifungulia, wodi ya mama na mtoto na wodi ya wanawake na wanaume pamoja na chumba cha kuhifadhia maiti.Uboreshaji huo unagharimu sh. milioni 500.

Waziri Mkuu alifungua mradi huo jana (Jumanne, Machi 19, 2019) akiwa ziarani Misungwi, ambapo aliwataka wananchi waendelee kuiunga mkono Serikali yao, ambayo imedhamiria kuwatumikia ili waweze kupata maendeleo.

“Hapa zamani kulikuwa na zahanati yenye jengo moja, tumeamua kuboresha na kupandisha hadhi na kuwa kituo cha afya. Rais Dkt. John Magufuli anataka wananchi wapatiwe huduma muhimu zikiwemo za afya karibu na makazi yao”.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alisema hakuna kijiji chochote nchini kitakachoachwa bila ya kuunganishiwa umeme katika awamu ya tatu ya Mradi wa Nishati Vijijini (REA), vikiwemo na vya wilaya ya Misungwi tena kwa gharama nafuu.

“Rais wetu Dkt. John Magufuli anajali sana wananchi wake, hivyo ametenga fedha nyingi zitakazotosheleza kusambaza umeme katika vijiji vyote vikiwemo na wilaya yenu hii ya Misungwi. Gharama za kuunganishiwa umeme huo ni sh. 27,000 tu.”

Waziri Mkuu aliongeza kwamba lengo la Serikali ni kufikisha umeme kwenye vijiji vyote Tanzania na vile ambavyo viko kwenye maeneo yaliyo mbali na gridi ya taifa vitafungiwa sola, jambo ambalo litafungua fursa za ajira na kukuza uchumi.

(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,


from MPEKUZI

Comments