Seikali yasimamisha biashara chuma chakavu

Serikali  imezuia biashara ya kuingiza na kusafirisha nje  ya nchi taka zenye madhara vikiwamo vyuma chakavu, betri zilizotumika na taka za  eletroniki mpaka utaratibu mpya utakapotolewa.

Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais   Dar es Salaam jana, imewataka watu wanaojihusisha na biashara ya ukusanyaji, usafirishaji, urejerezaji wa vyuma chakavu, taka za  elektroniki, taka za kemikali, mafuta machafu, taka zitokanazo na huduma za afya na betri zilizotumika kujiandikisha upya Baraza ka Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira na kupata vibali vipya kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais.

Utaratibu huo mpya utajumuisha ukaguzi wa uwezo wa waombaji wa kufanya shughuli hizo huku wafanyabishara wakionywa kutopokea taka hizo kutoka kwa mtu asiyekuwa na kibali kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais.

Taarifa hiyo ilitolewa   baada ya ziara ya ghafla ya Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba, katika Bandari ya Dar es Salaam.

Makamba  alitoa maelekezo na maagizo kuhusu utaratibu mpya wa biashara ya taka zenye madhara, baada ya kuwapo ukiukwaji wa Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004, kanuni za sheria hiyo na Mkataba wa Kimataifa wa Basel kuhusu taka zenye madhara.

Alisema Ofisi ya Makamu wa Rais inakusudia kubadilisha Kanuni za Usimamizi wa Mazingira za Mwaka 2009 na kuandika kanuni mpya za taka za  elekroniki kuweka udhibiti bora zaidi.

Wakati serikali ikitoa agizo hilo, tayari kuna makontena 44 ya vyuma chakavu katika Bandari ya Dar es Salaam na   Waziri Makamba na ujumbe wake wamekuta makontena 10.

“Lazima jambo hili lifuatiliwe kujua nani waliohusika na jambo hili wakati taarifa ya kusimamisha usafirishaji imekwisha kutolewa,” alisema.

Ilibainika kuwapo mzigo wa vyuma chakavu ulioingizwa nchini kwa majahazi  kama “loose cargo” kutoka Comoro kupitia Zanzibar.

“Tunawasihi wananchi wote pia kutoa taarifa haraka kwa mamlaka husika, ikiwamo NEMC na Ofisi ya Makamu wa Rais,  wanapohisi au kuona mtu au kampuni yoyote inaingiza nchini taka za aina yoyote kutoka nje ya nchi au ukusanyaji wa vyuma  chakavu, taka za elektroniki na betri zilizotumika na utupaji wa taka za hospitali unafanyika kinyume cha utaratibu,” alisema Makamba katika taarifa hiyo.

Katika ziara hiyo, Waziri Makamba aliambatana na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dk. Samuel Gwamaka na maofisa waandamizi wa baraza hilo.


from MPEKUZI

Comments